Watumishi wa Mamlaka
ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) Makao Makuu wamepatiwa mafunzo ya
namna mbalimbali za kukabiliana na kuchukua tahadhari dhidi ya majanga ya moto.
Akizungumza wakati wa
ufunguzi wa mafunzo hayo, tarehe 16 Juni 2022 kwenye ofisi za VETA Makao Makuu,
jijini Dodoma, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, amesema kuwa
uongozi umeamua kutoa mafunzo hayo kwa watumishi ili waweze kufahamu tahadhari
wanazopaswa kuchukua kuepuka majanga ya moto na njia sahihi za kukabiliana na
moto pindi unapotokea.
“Mafunzo haya ni muhimu sana kwetu wafanyakazi
kwa kuwa yanatusaidia kujenga ufahamu wa namna tunavyoweza kuzuia majanga ya
moto, lakini pia kukabiliana na moto pale unapotokea tukiwa ofisini na hata
majumbani kwetu,”amesema CPA Kasore.
Amewataka watumishi
hao kufanyia kazi mafunzo waliyoyapata ili kuepusha majanga ya moto ambayo
yanaweza kuzuilika na kuepusha madhara yanayotokana na moto.
Kwa upande wake Afisa
wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji jijini Dodoma, SSGT. Joyce Kapinga, amesema
bado kuna watu wengi hawafahamu njia sahihi za kukabiliana na majanga ya moto
kutokana na ukosefu wa elimu juu ya aina za visababishi vya moto na namna ya
kukabiliana na moto pale unapotokea.
Mafunzo hayo
yaliyotolewa kwa njia ya nadharia na vitendo yamehusisha watumishi 85 wa VETA
Makao Makuu kutoka idara mbalimbali.
No comments:
Post a Comment