Ujenzi
wa Chuo cha Ufundi Stadi cha Mkoa wa Rukwa umeanza rasmi baada ya makabidhiano
ya mradi huo kati ya Mamlaka ya Elimu na Mafunzo Stadi (VETA) na mkandarasi wa
mradi huo, kampuni ya Tendar International Ltd ya Kichina.
Makabidhiano
kati ya VETA na Mkandarasi wa ujenzi huo yalifanyika tarehe 30 Agosti, 2018
wilayani Sumbawanga na kuhudhuriwa na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Dkt Halfan
Haule.
Ujenzi
wa chuo hicho cha mkoa unatarajiwa kugharimu takribani kiasi cha bilioni kumi
(Bil. 10) na unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 12 na umelenga kukidhi
mahitaji ujuzi katika mkoa wa Rukwa na maeneo ya jirani.
Akizungumza
wakati wa makabidhiano ya mradi huo, Mwakilishi wa Kaimu Mkurugenzi VETA Adelina
Macha amesema dhamira ya VETA ni kujenga vyuo vya ufundi stadi kila mkoa ili
kuongeza udahili na uendelezaji ujuzi, hivyo kwenda sambamba na kasi ya
utekelezaji wa mkakati wa serikali kuelekea kwenye uchumi wa viwanda, kwani
VETA ina jukumu kubwa katika kuandaa nguvukazi kwa ajili ya uchumi viwanda.
Macha
amesema miongoni mwa vyuo vya hadhi ya mkoa ambavyo viko mbioni kujengwa ni
pamoja na Njombe, Geita, Simiyu, pamoja na Rukwa.
Akizungumza
kuhusu chuo hicho, Kaimu Mkurugenzi wa Soko la Ajira VETA, Hildergardis Bitegera amesema
kitakapokamilika kitakuwa na uwezo wa kudahili wanafunzi 600 kwa mwaka kwa
ngazi ya kwanza hadi ya tatu katika
mafunzo ya muda mrefu na wanafunzi wasiopungua 900 kwa mafunzo ya muda
mfupi.
Amesema
kuwa ujenzi huo utahusisha ujenzi wa karakana zitakazofundisha mafunzo kwa
vitendo katika kozi za ufundi
magari, uchomeleaji na uungaji vyuma, uhudumiaji na uuzaji wa vinywaji, ufundi
umeme, uandaaji na utayarishaji wa chakula, mafunzo ya ukatibu muhtasi, ubunifu
wa mavazi na ushonaji wa nguo, ufundi useremala , ufundi uashi, ukarimu na utengenezaji wa chakula.
Amesema
utafiti wa soko la ajira ulibaini kuwa shughuli kubwa za kiuchumi kwa wananchi
wa mkoa wa Rukwa ni kilimo, ufugaji na uvuvi, hivyo miongoni mwa kozi
zinazotarajiwa kufundishwa ni usindikaji wa chakula ili kuongeza thamani ya
mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi.
Akizungumza
wakati wa hafla ya makabidhiano hayo, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Dkt Halfan
Haule amesema kuwa Mkoa wa Rukwa ulikuwa na uhitaji wa Chuo cha mafunzo ya
Ufundi Stadi kwa muda mrefu, hivyo kuanza ujenzi huo kunaleta matumaini makubwa
kwa vijana na wananchi wengine mkoani humo kupata fursa za mafunzo ya ujuzi katika
eneo la jirani nao.
Aliishukuru
serikali kwa kuupa kipaumbele mkoa wa Rukwa na kuamua kujenga chuo cha Mkoa cha
Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi.
Aliongeza
kuwa matarajio ya serikali ni kuwa uwepo chuo hicho kutahamasisha maendeleo na
kuongeza kipato kwa wanacnhi katika mkoa wa Rukwa ambapo watafanya usindikaji
wa chakula pamoja na uhifadhi wa mazao.
Kaimu
Mkurugenzi wa Soko la Ajira VETA,
Hildergardis Bitegera akikabidhi mchoro wa ramani ya Jengo la Chuo VETA
Rukwa kwa Mkandarasi atakayejenga Chuo hicho.
Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Dkt Halfan Haule
akiwa katika picha ya pamoja Menejimenti
na watendaji wa VETA Makao Makuu, VETA Kanda ya Kusini Magharibi na Viongozi
mbalimbali wa Mkoa.
No comments:
Post a Comment