Walimu 56 wa fani ya
Ushonaji, Ubunifu na Teknolojia ya Nguo
kutoka vyuo vya VETA nchini wamepatiwa
mafunzo yenye lengo la kuwajengea uwezo katika kuboresha utoaji mafunzo, kufuatia
mabadiliko ya mitaala katika fani hiyo.
Akifunga mafunzo hayo
ya siku tatu yaliyofanyika katika ukumbi wa chuo cha VETA Dodoma, leo tarehe 27
Machi, 2024, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa
VETA, CPA Antony Kasore amesema mabadiliko makubwa yamefanyika katika mitaala
ya fani hiyo iliyohuishwa mwaka 2022, ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia
na mahitaji ya soko la ajira.
“Kupitia mafunzo haya, tunatarajia mkawe mawakili wema katika kuhakikisha kwamba ufundishaji unaendana na mabadiliko mitaala na kasi mabadiliko makubwa ya teknolojia na mahitaji ya soko la ajira kwa ujumla” amesisitiza.
Sambamba na kuwajengea uwezo katika eneo la mafunzo, CPA Kasore ameahidi kuwa Mamlaka itafanya juhudi za kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo kuwapatia mashine na vifaa vya kisasa vyenye uwezo wa kubeba uhalisia wa mahitaji ya kasi ya mabadiliko ya teknolojia katika ufundishaji.
“wito wangu kwenu
baada ya mafunzo haya na mara mtakapopokea vifaa na mashine hizo mtatusaidia
kuwaandaa wanafunzi na wahitimu watakaotangaza ubora wa fursa ya mafunzo katika
fani, hasa eneo la ubunifu, kujitangaza, kutafuta na kuchangamkia soko kupitia
mitandao mbalimbali, pamoja na kuwashirikisha wataalamu kutoka nje ili
wanafunzi wetu wahitimu wakiwa wenye tija zaidi”amesema
Akisoma risala kwa niaba ya walimu hao kwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu, Bi.Winifrida Ndunguru kutoka chuo cha VETA-Dakawa amesema, Mafunzo hayo yamewawezesha kupitia changamoto zote zilizokuwa zikiwakabili hasa kwenye eneo la mitaala mipya na kuzipatia ufumbuzi wenye uwelewa wa pamoja,kujifunza mbinu mpya za kupakua mawasilisho kwa njia ya elektroniki, kutumia TEHAMA na mifumo ya mitandao mbalimbali itakayowawezesha kupata zana za kufundishia na kujifunzia kwa nadharia na vitendo na kuahidi utekelezaji wake mara watakaporejea vituoni mwao.
Nae Bi. Anna Nyoni
aliemwakilisha Mkurugenzi wa mafunzo VETA Makao Makuu, amemshukuru Kaimu
Mkurugenzi Mkuu, kwa kuruhusu na kuona haja ya kuwepo kwa mafunzo hayo ambayo
yamefungua njia ya kutolewa kwa ufafanuzi wa mitaala ya kozi hiyo iliyohuishwa
mwaka 2022 pamoja na utekelezaji wake.