Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Prof. Adolf Mkenda, leo, tarehe 7 Mei 2026 amewasilisha Bungeni, Mpango na Bajeti wa Wizara hiyo huku akiainisha vipaumbele vitano vya mwaka wa fedha 2026/2027.
Katika hotuba yake Prof. Mkenda ameliomba Bunge kuidhinisha makadirio ya jumla ya Shilingi 2,394,423,829,000 ili kuwezesha utekelezaji wa malengo yaliyoanishwa na Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2026/27.
Prof. Mkenda ameainisha vipaumbele ambavyo Wizara hiyo itajielekeza kutekeleza kwa mwaka 2026/2027 kuwa ni pamoja na Kuendelea na utekelezaji wa sera na mitaala, mapitio ya sheria, kuandaa miongozo na kutoa mafunzo nchini; Kuongeza fursa na kuimarisha ubora wa mafunzo ya amali katika shule za sekondari na vyuo vya amali; Kuongeza fursa na kuimarisha ubora wa elimu ya awali, msingi, sekondari na ualimu; Kuongeza fursa na kuimarisha ubora wa elimu ya juu; na Kuimarisha uwezo wa nchi katika utafiti, matumizi ya sayansi, teknolojia na ubunifu ili kuchochea ujenzi wa uchumi wa viwanda.
Awali
akizungumzia utekelezaji wa mpango na bajeti ya mwaka 2025/2027 alitaja
mafanikio anuai ikiwa ni pamoja na ujenzi wa vyuo 65 vya VETA kufikia wastani
wa asilimia 68.
“Mradi huu wa kimkakati utaongeza fursa ya upatikanaji wa elimu ya ufundi katika ngazi ya wilaya, hivyo kuwezesha vijana wengi zaidi kupata ujuzi bila kulazimika kuhama maeneo yao. Hatua hii pia itaongeza usawa wa upatikanaji wa elimu nchini,” amebainisha.
Vilevile ameeleza kuwa Serikali imeanza utekelezaji wa Mfuko wa ‘Samia Innovation Commercialization Fund’, unaolenga kutoa mikopo yenye masharti nafuu kwa wabunifu ili kuwezesha ubidhaishaji na ubiasharishaji wa bunifu na teknolojia za wabunifu, ambapo katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa Mfuko wa ‘Samia Innovation Commercialization Fund’, wabunifu saba wamenufaika kwa kupata jumla ya Shilingi milioni 767.
Aidha, Prof. Mkenda amebainisha kuwa katika mwaka wa fedha 2025/2026 jumla ya wanafunzi 315,307 walidahiliwa, kati yao wanafunzi wa vyuo vya elimu ya ufundi ni 236,199 na vyuo vya mafunzo ya ufundi stadi ni 79,108 sawa na asilimia 119 ya lengo la kudahili wanafunzi 265,000.
Pia. Prof. Mkenda amesema kuwa Serikali, inatekeleza mpango wa kitaifa wa kuimarisha elimu ya ufundi na umahiri unaolenga kuandaa walimu wenye ujuzi wa kisasa na mbinu shirikishi za ufundishaji ambao umewezesha walimu 150 wa amali za kihandisi kwenda New Delhi, India kwa mwezi mmoja ambako walipatiwa mafunzo ya umahiri katika ufundishaji wa masomo ya amali na kupata fursa ya kushiriki mafunzo kwa vitendo katika shule za ufundi na ufundi stadi nchini humo.
“Ili kuandaa wahitimu wenye ujuzi na uwezo wa kujiajiri na kushindana katika soko la ajira kimataifa, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeandaa mpango wa pamoja kati ya waajiri, vyuo vya ufundi stadi na vyuo vikuu ambao ulizinduliwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Balozi Dkt. Emmanuel John Nchimbi tarehe 9 Februari, 2026 Jijini Dar es Salaam,” ameongeza.
Akiainisha kuhusu mpango wa mwaka 2026/2027, Prof. Mkenda alizitaja shabaha mbalimbali ambazo ni pamoja na kununua vifaa vya kufundishia na kujifunzia kwa ajili ya vyuo 145 vya VETA; kutoa mafunzo kwa walimu 6500 wa vyuo vya ufundi stadi na kusajili vyuo vya mafunzo ya ufundi stadi 152, hivyo kufikisha 1,066.
Shabaha zingine ni kudahili wanafunzi 134,000 wa vyuo vya mafunzo ya ufundi stadi, hivyo kuongeza idadi ya vijana wenye ujuzi na uwezo wa kujiajiri na kuajiriwa.
Vilevile, ameeleza kuwa kwa kutambua umuhimu wa mafunzo ya vitendo, Serikali itadahili walimu tarajali 200 katika Ndaki ya Mtwara ya Ualimu Ufundi ya Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya na walimu tarajali 1,000 katika Chuo cha Walimu wa Ufundi Stadi Morogoro.
Amesema, walimu tarajali watafundisha amali katika shule za sekondari za amali na vyuo vya mafunzo ya ufundi stadi na hivyo kuwezesha kuwa na wahitimu wenye uwezo wa kujiajiri au kuajiriwa na kutatua changamoto za kiufundi ambazo ndio msingi wa maendeleo ya kiuchumi wa taifa lolote linalotaka kujitegemea.
Pia ameseam Serikali itatoa mafunzo ya umahiri na mitaala inayozingatia teknolojia kwa watumishi wa VETA 6,500 na watumishi wa vyuo vya maendeleo ya wananchi 1,300 na kuwezesha mafunzo ya vitendo viwandani kwa watumishi 155 wa VETA na vyuo vya maendeleo ya wananchi.
Kuhusu mafunzo kwa wenye mahitaji maalum, Prof. Mkenda amesema Serikali itaendelea kuimarisha utoaji wa elimu kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum ikiwa ni pamoja na kuimarisha huduma ya ubainishaji na upimaji, pamoja na utoaji wa elimu nyumbani kwa wanafunzi kwa kutoa mafunzo kwa wakufunzi 100 kutoka VETA za mikoa na vyuo vya maendeleo ya wananchi kuhusu namna ya kuwahudumia wanafunzi wenye mahitaji maalum.
Bunge
limeanza kujadili na hatimaye linatarajiwa kuidhinisha Bajeti ya Wizara hiyo.

.jpeg)
.jpeg)




.jpeg)





.jpeg)









