CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Tuesday 18 September 2018

VETA yakabidhi vifaa vyenye thamani ya mil 41 kwenye chuo cha wenye ulemavu



Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imekisaidia chuo cha Ufundi kwa Watu wenye Ulemavu Yombo vifaa mbalimbali vya kufundishia vyenye thamani ya shilingi mil 41.4.


Akikabidhi vifaa hivyo jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Bodi ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi Kanda ya Dar es Salaam Dkt. Patricia Mwesiga alisema utoaji wa vifaa hivyo ni utekelezaji wa moja ya jukumu la VETA la kugharamia utoaji wa mafunzo ya ufundi stadi katika vyuo mbalimbali inavyovisimamia nchini.

Alisema vifaa hivyo vimetolewa  ili kuboresha utoaji wa mafunzo na kuongeza udahili kwa watu wenye ulemavu ili kuhakikisha vijana wenye ulemavu wanapata stadi mahiri zitakazowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo hasa katika kujenga uchumi wa viwanda.
Alisema serikali kupitia VETA inawathamini watu wenye ulemavu na kwamba itaendelea kushirikiana nao bega kwa bega kuhakikisha wanatimiza malengo yao bila kubaguliwa.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Dar es Salaam Florence Kapinga alivitaja vifaa hivyo kuwa ni pamoja na vyerehani vya kuendesha kwa mkono , vyerehani vya kuendesha kwa mguu, mashine ya nukta nundu, mashine za kuchomelea pamoja na vifaa vya kilimo, umeme na ujenzi vyenye thamani vitatumika katika fani za Umeme, Ushonaji,Uashi,Uungaji vyuma,Kilimo pamoja na ufugaji ambazo zinatolewa chuoni hapo.

Mkurugenzi huyo aliwataka wanafunzi na walimu kutumia vyema vifaa hivyo na kuvitunza ipasavyo ili kunufaisha vijana wengi zaidi watakaosoma katika chuo hicho.

Awali, Kaimu Mkuu wa Chuo cha Ufundi Yombo Mariam Chellangwa alisema vifaa walivyopatiwa vitasaidia kwa kiwango kikubwa sana kuboresha utoaji wa mafunzo chuoni hapo ambao umekuwa ukikabiliwa na changamoto nyingi.
Alisema chuo hicho kinakabiliwa na changamoto kubwa ya uhaba wa walimu pamoja na miundo mbinu ya kufundishia hali inayozorotesha utoaji wa mafunzo kwa ufanisi na kuongeza kuwa kati ya watumishi 23 wa chuo hicho idadi ya walimu ni watano pekee.

Mkuu huyo aliiomba serikali na wadau wengine kujitokeza na kushirikiana nao ili kuendelea kuboresha utoaji mafunzo ya ufundi stadi kwa watu wenye ulemavu nchini na kwa kuwa chuo hicho kinategemewa na watu wenye ulemavu kutoka nchini nzima .

Kuhusu uwezo wa udahili wa chuo hicho, Bi Chellangwa alisema chuo hicho kina uwezo wa kutoa mafunzo kwa vijana 150 kwa mwaka japo idadi ya wanafunzi chuoni hapo imeendelea kupungua mwaka hadi mwaka na kwa mwaka huu wana wanafunzi 68 pekee.

Mwanafunzi wa chuo hicho katika fani ya Kilimo na Ufugaji Buga Omari alisema vifaa walivyopatiwa vitasaidia kujifunza kwa vitendo zaidi fani hiyo na hatimaye kukamilisha malengo yake ya kuwa mkulima na mfanyabiashara wa mazao.

Alisema  uhaba wa walimu na miundo mbinu rafiki kwa watu wenye ulemavu imekuwa changamoto kubwa kwao katika kujifunza na kuomba serikali na wadau kujitokeza kusaidia chuo hicho.
 

No comments:

Post a Comment