CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Wednesday 23 December 2020

Mhe. Ulega aishirikisha VETA Mpango wa Kujenga Karakana za Mafunzo Wilayani Mkuranga

 

Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Mbunge wa Jimbo la Mkuranga, Mhe. Abdallah Ulega (Mb), amefanya mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Dkt. Pancras Bujulu, na kumuelezea juu ya mpango wake wa kujenga karakana za mafunzo ya ufundi stadi Wilayani Mkuranga.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika leo, tarehe 23 Desemba, 2020, katika ofisi za Makao Makuu ya VETA jijini Dar es Salaam, Mhe. Ulega amemuarifu Mkurugenzi Mkuu wa VETA juu ya mpango huo, ambapo analenga kushirikiana na wadau mbalimbali kujenga karakana za ufundi stadi Jimboni kwake ili kuwezesha vijana kujipatia ujuzi wa kuendesha shughuli mbalimbali za kichumi kwa ufanisi.

Mhe. Ulega ameiomba VETA kumpa ushirikiano katika mpango huo, kwa kumpa mwongozo juu ya vigezo na viwango vya karakana, vifaa, zana na mitambo ya kufundishia ili ujuzi watakaoupata vijana hao uwawezeshe kupata vyeti vya VETA na kutambuliwa rasmi kama mafundi stadi.

Mhe. Ulega anadhamiria kujenga karakana za fani mbalimbali, zikiwemo za Ufundi Umeme, Useremala, Uashi, Ufundi bomba na Uchomeleaji vyuma, hasa kwa kuzingatia kuwa fani hizo ndio zinaongoza kwa wingi wa fursa za ajira kwa vijana wengi Jimboni mwake.

Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu, amesema VETA imepokea ombi la Mhe. Ulega kwa uzito mkubwa na kwamba VETA itahakikisha inafanyia kazi ombi hilo na kulipa kipaumbele ili vijana wa Mkuranga waweze kupata ujuzi na kufanya shughuli zao kwa weledi. 

Mkurugenzi Mkuu ameshauri kuwa mafunzo kwa vijana hao yatolewe kwa mfumo wa Uanagenzi Pacha (Dual-Apprenticeship System, DATS), na hivyo amekiagiza Kitengo cha DATS cha VETA Makao Makuu kushirikiana naye katika kufanikisha azma yake hiyo.

Dkt. Bujulu amempongeza Mhe. Ulega kwa kutambua umuhimu wa mafunzo ya ufundi stadi na mchango wake katika kuwezesha vijana kujiajiri na kuleta maendeleo nchini.



No comments:

Post a Comment