CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Monday 1 March 2021

Makamu wa Rais aagiza vijana wa Tanga wapewe kipaumbele katika chuo cha VETA Korogwe


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan, ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa Chuo cha Ufundi Stadi cha Wilaya ya Korogwe na kuagiza uongozi wa mkoa wa Tanga na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kuhakikisha vijana wengi wa mkoa wa Tanga wanadahiliwa katika chuo hicho baada ya kukamilika.

Katika hafla hiyo iliyofanyika tarehe 15 Machi, 2021 katika eneo la Mtonga wilayani Korogwe, Mhe. Makamu wa Rais ameutaka uongozi wa mkoa wa Tanga kusimamia kwa karibu ujenzi wa chuo hicho ili kukamilika mapema na kuwezesha vijana wa mkoa wa Tanga kujiunga na kupata ujuzi wa aina mbalimbali.

Amesema Tanga ni miongoni mwa mikoa inayoshamiri kwa viwanda, hivyo kuna uhitaji wa nguvukazi yenye ujuzi na kwamba ni vyema nguvukazi hiyo ikatokana na vijana wa mkoa huo baada ya kuhitimu mafunzo ya ufundi stadi.

Awali akisoma taarifa ya mradi wa ujenzi wa chuo hicho, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt.Pancras Bujulu, amesema kuwa mradi huo ulianza kutekelezwa mwezi Machi, 2020 na umekadiriwa kugharimu kiasi cha shilingi 1.6 bilioni. 

Amesema mradi huo unatekelezwa na VETA kwa kutumia nguvukazi ya ndani (Force Account) kupitia Chuo cha VETA Kihonda kilichoko Morogoro.

Amesema chuo hicho kitakapokamilika kitakuwa na uwezo wa kudahili wanafunzi 240 kwa kozi za muda mrefu na wanafunzi 620 wa kozi za muda mfupi kwa mwaka.


No comments:

Post a Comment