CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Tuesday 15 June 2021

Prof. Nombo ahimiza ushirikiano na wadau, ubunifu, kukabiliana na changamoto za utoaji mafunzo ya ufundi stadi

Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Caroline Nombo, amewaelekeza watendaji wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kutumia ubunifu na kushirikiana na wadau mbalimbali katika kukabiliana na changamoto za utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi nchini.

Prof Nombo ametoa wito huo leo, tarehe 14 Juni 2021, alipotembelea Makao Makuu ya VETA kwa nia ya kupanua ufahamu wake juu ya shughuli zake, maendeleo na changamoto inazokabiliana nazo.

Akitoa taarifa juu ya shughuli za Mamlaka, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu, alisema licha ya mafanikio katika kupanua fursa na kuimarisha utoaji wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi nchini, VETA inakabiliwa na changamoto za uhaba mkubwa wa walimu na uchakavu wa vifaa vya mafunzo katika karakana za vyuo vyake, hasa vyuo vikongwe. 

Prof. Nombo aliipongeza VETA kwa juhudi inazofanya katika kuwawezesha Watanzania, husuani vijana, kupata ujuzi unaowapa fursa pana ya kuajiriwa au kujiajiri katika nyanja mbalimbali. “VETA ina umuhimu mkubwa sana katika maendeleo ya nchi yetu. Kwa hiyo ni muhimu kujipanga vizuri ili kuhakikisha elimu tunayoitoa inakidhi mahitaji. Licha ya kuifahamisha Serikali juu ya changamoto zinazowakabili, kuweni wabunifu na shirikianeni na wadau katika kukabiliana na changamoto ili kazi iendelee,” alisema.

Sambamba na hilo, Prof. Nombo alizungumzia umuhimu wa kuwafanya wenye viwanda kutambua kuwa wana wajibu wa kutoa nafasi za mafunzo kwa vitendo kwa vijana wanaojifunza ufundi stadi. Hii itawapa vijana wa VETA fursa ya kupata mafunzo yenye uhalisia viwandani na kutumia teknolojia ya kisasa ili kuwezesha uzalishaji nguvukazi mahiri kwa maendeleo ya viwanda.

Katika ziara yake, Prof. Nombo aliambatana na Mkurugenzi wa Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi Wizarani, Dkt. Noel Mbonde na Naibu Mkurugenzi wa Elimu ya Ufundi anayesimamia vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (FDC), Bi Magreth Issai.

Baada ya kuongea na Menejimenti ya VETA Makao Makuu, Naibu Katibu Mkuu alitembelea Chuo cha Ufundi Stadi na Huduma cha Mkoa wa Dar es Salaam na Chuo cha VETA cha TEHAMA Kipawa. Katika vyuo hivyo, NKM alitembelea Karakana mbali mbali za vyuo hivyo na kujionea jinsi mafunzo kwa vitendo yanavyotolewa kwa vijana wa VETA na shughuli mbali mbali za uzalishaji zinazoendeshwa katika karakana hizo.



No comments:

Post a Comment