CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday 22 September 2022

Katibu Mkuu Elimu ahimiza kipaumbele cha mafunzo ya ufundi stadi kiwe kuwezesha vijana kujiajiri

 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Francis Michael, amewataka watendaji wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kuhakikisha mwelekeo na kipaumbele cha utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi iwe ni kuwawezesha vijana kujiajiri, badala ya kutegemea kuajiriwa. 

Dkt. Michael ameyasema hayo, tarehe 21 Septemba, 2022, jijini Dodoma alipofanya ziara Makao Makuu ya VETA ikiwa ni mwendelezo wa ziara za kutembelea taasisi zilizo chini ya Wizara yake kwa ajili ya kufuatilia utekelezaji wa majukumu ya Taasisi hizo.

Dkt. Michael amesema kuwa Serikali imeweka kipaumbele kikubwa kwenye elimu ya ufundi stadi kwa kuwa ndilo eneo linaloweza kuwapatia vijana wengi ujuzi na maarifa ya kuwawezesha kutumia fursa zilizopo kujiajiri na kuendesha maisha yao.

 “Mheshimiwa Rais (Samia Suluhu Hassan) ametupa kipaumbele sana sisi VETA, kwa sababu elimu anayoitilia mkazo Mheshimiwa Rais ni elimu ya umahiri (Competence-Based) ambayo imeanzia VETA.  Mheshimiwa Rais anataka tunapowafundisha vijana wawe na elimu, ujuzi, maarifa, waweze kujiamini na kujiajiri,” amesema. 

Ameongeza kuwa mitaala ikiandaliwa na mafunzo kutolewa kwa kipaumbele cha kujiajiri, kuna fursa nyingi zipo katika jamii ambazo vijana wanaweza kuzitumia baada ya kuhitimu.

 “Mitaala iweze kuandaliwa katika namna ambayo kijana akitoka VETA, hata akiambiwa nataka kukuajiri aseme hapana, mimi nakwenda kujiajiri. Kuna fursa nyingi sana huko nje,” ameongeza.

Aidha Dkt. Michael amemshukuru Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kupanua wigo wa upatikanaji wa mafunzo ya ufundi stadi ambapo kwa sasa kazi kubwa ya ujenzi wa vyuo vya ufundi stadi kila Wilaya inaendelea ili kuhakikisha vijana wa kitanzania wanapata fursa ya kupata ujuzi wa kufanya kazi mbalimbali.

Awali akitoa taarifa ya utendaji kwa Katibu Mkuu, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, ameeleza kuwa miongoni mwa mafanikio katika mwaka uliopita ni pamoja na kudahili wanafunzi 90,712 katika vyuo vya VETA, miongoni mwao wakiwemo wa kike 31,033 na wenye mahitaji maalum 423; kufanya tafiti tisa (9) za soko la ajira katika maeneo ya Umeme, Uchapishaji, Upambaji, Uvuvi, Mitambo ya treni, Ujenzi, Biashara, Usafirishaji na Ufundi wa Magari.

Ameyataja mafanikio mengine kuwa ni ujenzi vyuo vipya vya VETA, vikiwemo vyuo 25 vya wilaya vilivyojengwa na VETA kwa kutumia nguvukazi ya ndani; uratibu wa ujenzi wa chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi na Huduma cha mkoa wa Kagera ambacho kilikuwa kikijengwa kwa msaada wa Serikali ya China; uratibu na ufuatiliaji wa ujenzi na upanuzi wa vyuo vingine ambavyo ni pamoja na Chuo cha VETA Karagwe, Nyasa, Kongwa, Kasulu, Ruangwa, Nyamidaho, Njombe, Geita, Simiyu na Rukwa. Pia VETA ilifanya upanuzi na ukarabati wa miundombinu ya Chuo cha Ualimu wa Ufundi Stadi Morogoro (MVTTC), Chuo cha Hoteli na Utalii cha VETA Arusha (VHTTI), Chuo cha Ufundi Stadi Busokelo na Chuo cha Ufundi Stadi na Huduma cha Mkoa wa Arusha. Pia jumla ya wabunifu 277 kutoka vyuo vya ufundi stadi na mfumo usio rasmi walitambuliwa kupitia Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU).

Katika ziara hiyo, Katibu Mkuu katika aliambatana na Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia  Ndg. Moshi Kabengwe.





No comments:

Post a Comment