CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday 17 November 2022

Prof. Mkenda: Wekeni mikakati ya kutafsiri kwa vitendo maono ya elimu ujuzi


Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mheshimiwa Prof. Adolf Mkenda, amewaasa na kuwakumbusha watendaji wa Wizara hiyo na taasisi zake kuweka na kutekeleza mikakati mbalimbali yenye kutafsiri kwa vitendo maono ya nchi kuhusu elimu ujuzi.

Prof. Mkenda ametoa wito huo wakati wa kikao cha pamoja kati ya menejimenti na watendaji waandamizi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), kilichofanyika kwenye Chuo cha VETA Dodoma, leo tarehe 17 Novemba 2022.

Kikao hicho kilikuwa kikitathmini utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa vyuo 25 vya ufundi stadi vya wilaya, awamu ya kwanza, sambamba na kujadili mkakati wa ujenzi wa vyuo vya ufundi stadi kwenye wilaya 63 katika awamu ya pili.

Amewaasa kufanya kazi kwa kuzingatia matokeo ili utekelezaji wa maono ya elimu ujuzi uonekane wazi.

"Nchi yote sasa inazungumza kuhusu elimu ujuzi ambapo kiuhalisia ni ufundi stadi. Hivyo, sisi tuna jukumu kubwa la kutafsiri na kuonesha matokeo zaidi," amesema.

Akizungumza kuhusu mkakati wa ujenzi wa vyuo vipya 63 vya ufundi stadi vya wilaya, Prof. Mkenda amewaagiza watendaji kufanya upembuzi wa kina juu ya namna bora ya kutekeleza, ikiwemo kupima faida na changamoto za kutumia nguvukazi ya ndani (Force Account); kutumia wakandarasi au kukabidhi taasisi zingine za Serikali.

Awali, wakati akiwasilisha taarifa kwa Waziri, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA. Anthony Kasore, alisema kuwa ujenzi wa vyuo 25 vya ufundi stadi vya wilaya uliokuwa ukitekelezwa na VETA kwa kutumia Force Account uko katika hatua za mwisho na unatarajiwa kukamilika ifikapo Desemba mwaka huu.

Sambamba na ujenzi, VETA pia ilikuwa ikitengeneza samani za vyuo hivyo kupitia karakana zake ambapo alisema kuwa utengenezaji wake umefikia asilimia 90 na kwamba karibu nusu ya samani zimeshasambazwa kwenye vyuo vipya vya VETA.

Kuhusu ujenzi wa vyuo 63 vya awamu ya pili, CPA Kasore amewasilisha mapendekezo ya ujenzi ikiwemo wilaya ambazo zimeleta maombi na kueleza kuwa baadhi zimeshatenga maeneo kwa ajili ya ujenzi huo.

No comments:

Post a Comment