CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Friday 11 November 2022

VETA yaikabidhi Wizara ya Elimu mitaala ya mafunzo ya ufundi shule za msingi

 

Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imeikabidhi Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia mitaala 10 na mihutasari minne ya ufundi kwa ajili ya shule za msingi zenye mikondo ya ufundi (Post Primary Technical CentresPPTC).

Mitaala hiyo imekabidhiwa kwa Kamishna wa Elimu nchini Dkt. Lyabwene Mtahabwa na Mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA. Steven Kwetukia, kwenye kikao cha Kamati ya Kitaifa ya utekelezaji wa mradi wa Elimu Bora kwa Ukuaji wa Afrika Awamu ya Pili, (Better Education for Africa’s Rise-Phase Two-BEAR II) kilichofanyika jijini Dar es Salaam tarehe 10 Novemba, 2022.

Mradi wa BEAR II uliofadhaliwa na UNESCO na Serikali ya Korea ulilenga kuongeza ubora na umuhimu wa Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (TVET) na kubadili mtazamo juu ya elimu hiyo ambapo utekelezaji wake umefanyika kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia 2020 hadi 2022.

Mkurugenzi wa Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA, Ndugu Abdallah Ngodu, ameainisha mitaala iliyotengenezwa na kukabidhiwa kuwa ni ya masomo ya Uchumi wa Nyumbani, Kilimo cha Bustani, Useremala, Umeme wa Majumbani, Ufugaji, Uchomeleaji Vyuma, Uashi, Ufundi Magari, Ufundi Bomba na Kazi za Mikono. Pia VETA imeandaa mihtasari ya masomo ya Kiswahili, Kingereza, Hesabu na Uraia.

Ndugu Ngodu ametaja mafanikio yaliyopatikana kupitia mradi huo kuwa ni pamoja na uandaaji wa Mitaala ya uchakataji wa chakula na Upangaji na Upambaji wa Mazingira ya Ndani ya Nyumba (Interior Design) kwa ngazi ya 4 hadi 6 za elimu ya ufundi, pamoja na uwezeshaji vifaa vya kisasa vya mafunzo ya uchakataji wa vyakula kwa chuo cha Ualimu wa Ufundi Stadi Morogoro (MVTTC). Kupitia mradi wa BEAR II watumishi wa MVTTC walipatiwa mafunzo kuhusu masuala mbalimbali ya kiutendaji, utawala bora na mpango mkakati pamoja na kuwezeshwa vifaa vya TEHAMA kwa ajili ya kuimarisha mafunzo kwa Masafa kidigitali kwenye chuo hicho. 

Amesema shughuli nyingine zilizofanywa na VETA ni kufundisha wakulima wa Halmashauri za Wilaya za Morogoro, Mvomero na Manispaa ya Morogoro kuhusu mnyororo wa thamani katika zao la muhogo,   Uaandaji wa Sherehe na Upambaji.

No comments:

Post a Comment