CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Monday 21 November 2022

Wananchi Mbarali waanza kunufaika na mafunzo ya ufundi stadi kupitia chuo kipya cha VETA Wilayani humo

 

Wananchi wilayani Mbarali mkoa wa Mbeya wameanza kunufaika na mafunzo ya ufundi stadi katika chuo kipya cha VETA wilayani humo, ambapo tayari wananchi 35 wamehitimu mafunzo ya muda mfupi katika chuo hicho. 

Hafla ya kukabidhi vyeti wahitimu hao katika fani za  Uashi na Udereva imefanyika tarehe 19 Novemba 2022 ambapo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali, Ndugu Missana Kwangura amewatunuku vyeti.

Mafunzo hayo yametolewa kupitia jitihada za Mkurugenzi huyo za kuhakikisha wananchi wa Wilaya ya Mbarali wanapata stadi zinazohitajika Wilayani hapo katika kufanikisha shughuli mbalimbali za kiuchumi. 

Wahitimu hao walipatiwa mafunzo kwa mwezi mmoja kuanzia tarehe 21 Septemba hadi 21 Oktoba, 2022 ambapo wananchi 27 kati yao walifundishwa udereva na nane uashi.

Msimamizi wa chuo hicho ambaye pia ni Mkuu wa Chuo cha VETA Mbeya, Mhandisi Hassan Kalima, amesema kwenye fani ya uashi wananchi hao wamefundishwa kutengeneza tofali bora za saruji kwa ajili ya ujenzi wa miradi mbalimbali ya Serikali wilayani hapo.

Chuo cha Ufundi Stadi cha Wilaya ya Mbarali ni miongoni mwa vyuo vipya 25 vilivyojengwa na VETA kwa kutumia nguvukazi ya ndani (Force account). Chuo hicho kinatarajia kuanza kutoa mafunzo ya muda mrefu mwezi Januari, 2023 katika fani za Ushonaji, Umeme wa Majumbani pamoja na Uhazili na Kompyuta.

No comments:

Post a Comment