CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Saturday 3 December 2022

DC Shekimweri aishauri VETA kushirikiana na wadau, ujenzi wa hosteli za wanafunzi

 

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Mhe. Jabir Shekimweri, ameishauri Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kushirikiana na taasisi za ujenzi nchini kuwezesha ujenzi wa hosteli za wanafunzi ili kukabiliana na changamoto ya makazi kwa wanafunzi iliyopo kwenye vyuo vingi vya VETA nchini.

Akizungumza wakati wa mahafali ya 39 ya Chuo cha VETA Dodoma leo tarehe 3 Desemba, 2022, Mhe. Shekimweri amesema kuwa ujenzi wa hosteli za kutosheleza mahitaji ya wanafunzi utawezesha wanafunzi wa ufundi stadi kupata mafunzo yao kwa ufanisi zaidi.

“NI wakati sasa VETA ifikirie kufanya makubaliano ya mashirikiano na Taasisi za ujenzi kama TBA na NHC ili Taasisi hizi zijenge hosteli za kutosheleza mahitaji ya wanafunzi na kuziendesha kwa muda fulani na baadaye zikabidhiwe VETA,”amesema

Uhaba wa hosteli zinazotosheleza idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa kwenye vyuo vya VETA ni miongoni mwa changamoto zilizowasilishwa na wahitimu wa mafunzo ya ufundi stadi kwenye hotuba yao waliyoisoma kwa Mgeni Rasmi wa mahafali hayo Mhe. Shekimweri.

Aidha, Mhe Shekimweri ameahidi kuratibu vikundi vya wahitimu wa fani mbalimbali chuoni hapo kupata mikopo ya asilimia 10 inayotengwa na Halmashauri ili waweze kujiajiri.


Mkurugenzi wa Utahini na Utunuku wa VETA, Ndugu Francis Komba, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa VETA kwenye mahafali hayo, amesema VETA imeendelea kuhakikisha ubora wa mafunzo yanayotolewa kwenye vyuo vyake ili kuzalisha nguvu kazi mahiri yenye ujuzi unaohitajika kwenye soko la ajira.

 

Awali Mkuu wa Chuo cha VETA Dodoma, Ndugu Stanslaus Ntibara, amesema chuo chake kinashirikiana na wadau wa ndani na nje ya nchi katika kutoa mafunzo ya ufundi stadi kwa makundi mbalimbali na kuyawezesha makundi hayo kushiriki kikamilifu kwenye shughuli mbalimbali za uchumi.

“Baadhi ya wadau tulioshirikiana nao katika mwaka wa masomo unaokwisha ni pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu (Ufadhili wa Wanagenzi 586), Wizara ya Kilimo (Wanagenzi 60), Taasisi ya Elimu Tanzania (TEA) Wanagenzi (407), Shirika la Maendeleo la Ujerumani (GIZ) na Shirika la Maendeleo la KOREA Kusini (KOICA) chini ya mpango wa E4D (Wanafadhili wanafunzi 2,200),”amesema

Mahafali hayo yamehusisha jumla ya wahitimu 493 wa mafunzo ya ufundi stadi kati yao 258 wamehitimu katika fani za muda mrefu hatua ya pili (level II) na ya tatu (level III) na 235 wamehitimu mafunzo ya uwanagenzi yaliyotolewa kwa muda wa miezi sita kupitia ufadhili wa ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana,Ajira na Wenye Ulemavu.

Wahitimu hao wamesoma fani za Useremala,Upishi,Ufundi Bomba, Uungaji na Uchomeleaji Vyuma, Umeme wa Majumbani, Ukarabati na Ujenzi wa Barabara, Uchinjaji na Uchakataji wa Nyama, Upakaji Rangi na Uandishi wa Alama, Elektroniki,Ukerezaji wa Vyuma, Uashi, Huduma ya Mapokezi, Ufundi Magari pamoja na Uhudumu na Uuzaji wa Vyakula na Vinywaji.

No comments:

Post a Comment