Katibu Mkuu wa Wizara
ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Francis Michael, ameipongeza Bodi ya Nane
ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi kwa usimamizi thabiti wa elimu na mafunzo
ya ufundi stadi nchini.
Akizungumza wakati wa
hafla ya kuiaga Bodi hiyo jijini Dodoma tarehe 9 Januari, 2023, Dkt. Michael
amesema miongoni mwa mambo yaliyosimamiwa vyema na Bodi hiyo ni ujenzi wa vyuo
vya ufundi stadi vya wilaya ambao umetekelezwa na VETA kwa kutumia nguvukazi ya
ndani, pamoja na ubunifu wa programu za mafunzo kwa kuzingatia mahitaji ya soko
la ajira na mwenendo wa nchi kiuchumi.
“Itoshe kusema kwamba
usimamizi wenu ulikuwa mzuri na mmeitendea vyema mipango mbalimbali ya VETA, hasa
Mpango Mkakati wa Tano (VCP V) wa mwaka 2018/2019 hadi 2022/2023 ambao ndo hasa
ulikuwa katika kipindi chetu cha usimamizi wa VETA… hongereni sana. ,” amesema.
Amesema Serikali ya
Awamu ya Sita imeipa kipaumbele kikubwa sana elimu na mafunzo ya ufundi stadi
na kwamba uendeshaji na usimamizi wake unapaswa kuwa imara na madhubuti.
Awali, Kaimu
Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA. Anthony Kasore, amesema katika kipindi cha
kuanzia mwezi Februari, 2020, VETA imepata mafanikio mbalimbali ikiwemo
uandaaji wa mitaala 54 kuendana na mahitaji ya soko la ajira, uanzishwaji wa
vyuo vipya 19 pamoja na utanuzi wa miundombinu 31 kwenye vyuo vya VETA nchini
na kuongeza udahili wa wanafunzi kwenye vyuo vya VETA kutoka 56,000 mwaka 2020
hadi 141,854 mwaka 2023.
Mwenyekiti wa Bodi ya
Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Ndugu Peter Maduki, ameishukuru Serikali kwa
kuiamini Bodi hiyo na kuipa ushirikiano mkubwa katika kutekeleza majukumu yake
na hatimaye kuiwezesha VETA kupiga hatua katika utoaji wa mafunzo ya ufundi
stadi.
No comments:
Post a Comment