Mamlaka ya Elimu na
Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imejipanga vyema kuhakikisha watanzania wengi
zaidi wananufaika na mafunzo bora ya ufundi stadi yanatolewa kupitia vyuo vyake
nchini kote.
Akitoa salamu za
mwaka mpya kwa Watanzania jijini Dodoma tarehe 4 Januari, 2023, Kaimu
Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, alisema kwa mwaka 2023 VETA
imedhamiria kuongeza fursa zaidi za mafunzo ya ufundi stadi kwa watanzania ili kuwawezesha kujipatia
ujuzi utakaowawezesha kushiriki kikamilifu kwenye shughuli mbalimbali za
uchumi.
CPA. Kasore ametaja
baadhi ya matarajio ya Mamlaka hiyo kuwa ni kuongeza udahili wa wanafunzi
kutoka 90,000 kwa mwaka 2022 hadi 118,000 kwa mwaka 2023 na kumalizia ujenzi wa
vyuo 25 vya ufundi stadi vya Wilaya pamoja na kuratibu ujenzi wa vyuo vipya 64 vya Wilaya na chuo cha Mkoa wa Songwe.
“Tumejipanga vyema
kuhakikisha kuwa ujenzi wa vyuo vya ufundi stadi vya Wilaya 63 nchini na ujenzi
wa chuo cha ufundi stadi na huduma cha Mkoa wa Songwe unatekelezwa kwa ufanisi…
Tunashukuru Serikali imeshatenga shilingi bilioni 100 katika mwaka wa fedha
2022/2023 kwa ajili ya kuanza ujenzi huo,” alisema.
Akizungumza kuhusu
mafanikio yaliyopatikana mwaka 2022, CPA Kasore alitaja baadhi ya mafanikio
kuwa ni pamoja na kukamilisha kwa asilimia 97 ujenzi wa vyuo 25 vya Wilaya kwa
kutumia nguvu kazi ya ndani yaani “Force Account” na uratibu wa ujenzi wa vyuo
vinne vya Mikoa ya Simiyu, Njombe, Geita na Rukwa.
Katika kuhakikisha mafunzo ya ufundi stadi yanatolewa kwa ubora, CPA Kasore alisema katika mwaka 2022, jumla ya mitaala 48 ilihuishwa ili kuendana na mahitaji halisi ya soko la ajira na kuakisi mabadiliko ya sayansi na teknolojia.
Aidha, CPA Kasore
alisema VETA imeendeleza ushirikiano na wadau mbalimbali ili kuwafikia
watanzania wengi zaidi wenye mahitaji ya mafunzo ya ufundi stadi na kukidhi
mahitaji ya makundi mbalimbali kwenye jamii.
Alitaja baadhi ya
wadau hao kuwa ni Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu
kupitia mradi wa Uwanagenzi ambapo jumla ya vijana 3900 walipatiwa mafunzo na
Shirika la Maendeleo ya Ujerumani (GIZ) kupitia mradi wa E4D kutoa mafunzo kwa
vijana 4200 nchini.Wanufaika wote hao walipatiwa mafunzo hayo bila malipo.
CPA Kasore alitoa
shukrani kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa Mhe. Dkt. Samia Suluhu
Hassan kwa kuendelea kutoa kipaumbele kikubwa kwenye elimu na mafunzo ya ufundi
stadi ili kuhakikisha watanzania wanajipatia ujuzi utakaowawezesha kushiriki
kwenye shughuli mbalimbali za kiuchumi na kuwezesha vijana kujiajiri.
“Mhe. Rais amekuwa na
malengo makubwa sana katika kuhakikisha elimu ya ufundi stadi inaimarika na
kutolewa ndani ya nchi na tumeshuhudia mengi yakifanyika kwenye eneo la
kuboresha miundombinu inayotumika kutoa mafunzo ya ufundi stadi… Tunamshukuru
sana,” Amesema
Kwa mujibu wa CPA
Kasore, moja ya changamoto inayoikabili Mamlaka hiyo ni kushindwa kuhimili
idadi kubwa ya watanzania wanaoomba nafasi za kupata mafunzo ya ufundi stadi
kwenye vyuo vya VETA ambayo anaamini itatatulia kwa kiasi kikubwa na ujio wa vyuo
vya Wilaya na Mikoa, huku Mamlaka hiyo ikiendelea kubuni njia mbadala za utoaji
mafunzo kwa watanzania.
No comments:
Post a Comment