CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Wednesday 23 August 2023

KONGAMANO LA UJUZI NA AJIRA KUWAKUTANISHA WANAFUNZI, WAHITIMU WA VETA NA WAAJIRI

 

Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) ikishirikiana na Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Ujerumani (GIZ) kupitia programu ya Kukuza Ajira na Ujuzi kwa Maendeleo Afrika (E4D), wameandaa Kongamano la Ujuzi na Ajira (Job and Skills Fair) lenye kauli mbiu isemayo “Ufundi Stadi kwa Fursa zaidi za Ajira” linalotarajiwa kufanyika katika viwanja vya Nyerere Square, tarehe 24 Agosti, 2023, jijini Dodoma.

Akizungumza na waandishi wa habari,katika ofisi za VETA Makao Makuu jijini Dodoma leo tarehe 22 Agosti,2023, Mkurugenzi wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi -VETA, Ndg. Abdallah Ngodu aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa VETA amesema kongamano hilo limelenga kuwajengea wananchi uelewa juu ya fursa za Ufundi Stadi zitolewazo kupitia mradi wa E4D,kukuza uwezo wa kujiajiri na kuajiriwa kwa wanufaika wa kozi zilizotolewa katika vyuo vya VETA nchini chini ya mradi huo.

Ameongeza kuwa wanufaika wa mradi huo watakutanishwa na Waajiri ili kushirikishana taarifa za soko la Ajira kwa ambapo hadi sasa jumla ya Makampuni na viwanda 20 vimethibitisha kushiriki kwa kuonesha bidhaa na huduma zao lakini pia watapata fursa ya kuthibitisha uhalisia wa umahiri na ujuzi wa wahitimu wa Mafunzo ya Ufundi Stadi yatolewayo na VETA.

“Kongamano hili litawapa fursa wananchi ya kujionee shughuli zifanywazo na wahitimu/wanufaika wa mradi wa E4DT pamoja na kupata taarifa juu ya fursa za Mafunzo ya Ufundi Stadi zitolewazo katika vyuo vya VETA nchini” amesema.

Amesema hadi sasa jumla ya vijana 3,258 wamenufaika na mafunzo katika fani za Ufundi Bomba  wa majumbani, Ufundi Bomba Viwandani na Ufundi wa Uchomeleaji Vyuma Viwandani (Industrial Welding) katika vyuo vya VETA vya Dodoma, Manyara. Lindi na Manyara.

Kwa upande wake, Mshauri wa Programu wa Shirika la GOPA aliyewakilisha washirika wa Mradi, Bi Leah Dotto. amesema utekelezaji wa programu hiyo umekuwa na mafanikio kwa kuwa umewezesha vijana kujipatia ujuzi na baadhi yao wameweza kuajiriwa na wengine kujiajiri

Tanzania ni miongoni mwa nchi sita za Afrika zinazotekeleza mradi wa Stadi za Ajira kwa Maendeleo Afrika (E4D) unaofadhiliwa na Wizara ya Shirikisho la Ujerumani la Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo (BMZ) na Shirika la Ushirikiano wa Maendeleo la Korea (KOICA). Mradi huo ulianza kutekelezwa mwezi Mei, 2022, ukilenga kutoa mafunzo ya muda mfupi kwa vijana 4000 nchini ili kuandaa nguvu kazi itakayotumika katika kukuza ajira kwenye miradi ya kimkakati inayotekelezwa hapa nchini.



 

No comments:

Post a Comment