CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday 31 August 2023

Vijana wa kike 221 kutoka mazingira magumu wahitimu mafunzo VETA Kishapu

 


Vijana 221 kutoka katika mazingira magumu wamehitimu mafunzo maalum ya ufundi stadi katika Chuo cha VETA cha Wilaya ya Kishapu kupitia ufadhili wa shirika lisilo la kiserikari la Wanawake katika Sheria na Maendeleo Barani Africa (WiLDAF) kwa kushirikiana na Shirika la Idadi ya Watu Duniani (UNFPA), pamoja na serikali ya Finland.

WiLDAF imewezesha vijana wa kike waliofanyiwa ukatili, kupewa mimba za utotoni na wenye ulemavu kupata mafunzo hayo kupitia mradi wake wa “Chaguo Langu Haki Yangu”

Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Kaimu Mkurugenzi wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Abdallah Ngodu, lengo la ujenzi wa vyuo vya VETA ikiwemo chuo cha VETA cha Wilaya ya Kishapu ni kupanua fursa za upatikanaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi nchi nzima na kwa makundi mbalimbali, ili kuandaa nguvu kazi yenye ujuzi wa kutosha kulingana na mazingira yaliyopo.

Amewaasa wahitimu hao kutumia fursa hiyo kuleta maendeleo katika jamii na kuwa mabalozi kwa mabinti wengine huko katika jamii.

 “VETA tumeamua kusogeza huduma karibu na wananchi ili wananchi wengi waweze kujiunga na kupata mafunzo haya ya ufundi stadi na tunaamini kwa hapa Kishapu mmeona umuhimu wa uwepo wa chuo hiki, hivyo tunaomba muendelee kushirikiana na chuo hiki kwa kuwaeleza wananchi umuhimu wa mafunzo yanayotolewa,” ameongeza Ngodu

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo cha VETA Shinyanga, Magu Mabelele, ambaye ni msimamizi wa Chuo hicho amesema kati ya vijana 221 waliodahiliwa, 101 walijiunga na Ushonaji; 39 Urembo na Mapambo; 20 Uhazili na TEHAMA, 1Uchomeleaji na Uungaji Vyuma, 7 Udereva wa Magari, 22 Ufundi Umeme, 3 Ufundi Magari, 11 Ufundi Bomba, 12 Upishi na Uandaaji Chakula na 5 Kudarizi.

Amesema, licha ya kusaidia kuwapatia ujuzi vijana hao, kupitia mradi huo, VETA imenunua vifaa vyenye thamani ya zaidi ya milioni 30,250,000, vikiwemo vyerehani 70; vifaa kwa ajili ya mafunzo ya urembo (saluni) na vifaa kwa ajili ya mafunzo ya umeme.

Mabelele amesema kutokana na ununuzi wa vifaa katika chuo hicho, VETA imepanga kuanzisha kozi za muda mrefu katika fani za Ushonaji, Ubunifu wa Mavazi na Teknolojia ya Nguo na Ufundi umeme, ambazo zitaanza kutolewa Januari 2024.

 “Kupitia mradi huu wa “Chaguo langu haki yangu” vijana hawa wameweza kubadilishiwa mtazamo wa kimaisha hasa katika jamii wanapokwenda, kwani tayari wana uwezo wa kuajiriwa au kujiajiri,” Ameongeza.

Naye Mkurugenzi wa Shirika la wanawake katika Sheria na Maendeleo Afrika WiDAF Bi. Anna Kulaya amesema, kuhitimu kwa mabinti hao kunatoa hamasa kwa shirika lake kuendelea kutafuta wafadhili wengine zaidi ili kusaidia mabinti wengi zaidi kuweza kupata fursa ya kupata mafunzo ya ufundi stadi.

Amesema kuwa kupita mafunzo hayo, mabinti wengi wameweza kufufua ndoto zao na kupata matumaini mapya ya maisha na kuongeza kuwa anaamini mabinti hao wanaweza kujiajiri au kuajiriwa na pengine kufungua biashara zao mbalimbali ikiwemo kwenye upishi na biashara ndogo ndogo.

Baadhi ya wanafunzi wahitimu wa mradi huo wamepongeza na kushukuru kupata mafunzo hayo na kuahidi kwenda kuwa mabalozi katika jamii zinazowazunguka.

 “Mimi nimejifunza kitu kikubwa sana kupitia mafunzo haya, nina hakika nikitoka hapa ninaenda kujitegemea mwenyewe na sitakuwa tegemezi kama ilivyokuwa kipindi cha awali,” Amesema Naomi Jonas, Mhitimu katika fani ya Ufundi Bomba.


Awamu ya kwanza ya mradi wa Chaguo Langu Haki Yangu” ilitekelezwa katika mikoa ya Mara na Shinyanga, wilaya za Kahama, Butiama na Kishapu.











No comments:

Post a Comment