CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Monday 23 October 2023

SHELL, EQUINOR ZAWEZESHA VIJANA LINDI KUPATA UJUZI


Makampuni ya Kimataifa ya Shell na Equinor yameunga mkono juhudi za Serikali kuwezesha vijana kupata ujuzi na kuongeza fursa za kuajirika kwa kutoa ufadhili kwa vijana 24 mkoani Lindi kujifunza fani mbalimbali za ufundi stadi Ngazi ya Tatu (Level 3).

Ufadhili wa makampuni hayo umehusisha ada, bima ya afya, malazi, chakula, usafiri pamoja kutoa vitendea kazi kwa wahitimu ili kuwawezesha kujiajiri mara baada ya kuhitimu mafunzo.

Akizungumza wakati wa mahafali ya wahitimu ya wahitimu hao, yaliyofanyika tarehe 13 Oktoba, 2023 kwenye Chuo cha VETA Lindi, Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Shaibu Ndemanga, aliyemwakilisha Mkuu wa mkoa wa Lindi, alisema ufadhili huo umelenga kuwaandaa wahitimu hao kuweza kujiajiri pamoja na kupata nguvu kazi yenye ujuzi utakaotumika katika miradi ya Kimkakati ya Gesi mkoani Lindi.

Ndemanga aliyashukuru makampuni hayo kwa kufadhili mafunzo na kuwaomba kupanua wigo wa ufadhili huo kwa wanafunzi wa ngazi ya kwanza na ya pili.

Aliwasihi wahitimu kwenda kujiunga katika vikundi ili kuwarahisishia kupata mikopo itakayowasaidia kuendeleza miradi ya uzalishaji.

Akisoma taarifa ya chuo kwa mgeni rasmi, Kaimu Mkuu wa Chuo cha VETA Lindi, Harry Mmari, alisema mafunzo hayo yamechukua muda wa mwaka mmoja, ambapo vijana walipata ufadhili kwa asilimia 100 kwa kulipiwa ada, bima ya afya, malazi, chakula, usafiri pamoja na kupatiwa vitendea kazi vya kwenda kujiajiri mara baada ya kuhitimu na kufaulu mafunzo yao.


Ufadhili wa kampuni hizo umetolewa kwa wahitimu wa kozi za umeme wa majumbani wanafunzi 11, Mafunzo ya kozi ya vioyozi na majokofu wanafunzi 4, kozi ya Ufundi Magari wanafunzi 4, kozi ya Uashi wanafunzi 4 na mwanafunzi 1 katika kozi ya Uchomeleaji na Uungaji vyuma.


No comments:

Post a Comment