CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday 21 March 2024

KAMATI YA BUNGE YAPONGEZA UTOAJI MAFUNZO YA UANAGENZI CHUO CHA VETA MWANZA

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii, imepongeza utoaji mafunzo ya uanagenzi katika chuo cha VETA Mwanza, kupitia ufadhili wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi,Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu.

Pongezi hizo zimetolewa Jijini Mwanza, tarehe 19 Machi, 2024, wakati wa ziara ya Kamati hiyo kukagua utekelezaji wa mafunzo ya ukuzaji ujuzi kwa njia ya Uanagenzi katika chuo cha VETA Mwanza.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Fatuma Hassan Toufiq, amesema kazi kubwa ya kamati yake ni kuangalia na kukagua utekelezaji wa miradi ambayo Serikali imetoa fedha ili kuona thamani ya fedha katika miradi hiyo.

 “Katika chuo hiki tumefarijika sana kuona vijana mbalimbali wakipatiwa mafunzo…tumepita katika karakana tumejionea vijana wa kike na kiume wakijifunza namna ya kuwa mafundi wa aina mbalimbali kama vile mafundi bomba, mafundi umeme, useremala na wengine wengi,” amesema.

Wakiwa kwenye karakana za mafunzo, wajumbe hao waliwapongeza vijana kwa umahiri wa kuonesha na kuelezea kile walichojifunza na bidhaa mbalimbali walizozalisha kutokana na mafunzo.


Mhe. Toufiq amewataka vijana waliopata mafunzo ya kukuza ujuzi kwa njia ya uanagenzi katika chuo cha VETA Mwanza kuhakikisha wanatumia vyema ujuzi wao ili kuwaletea tija katika shughuli zinazohusiana na ufundi stadi, hivyo kuwawezesha kujikwamua kiuchumi.

Amesema Kamati hiyo itaishauri Serikali kuona uwezekano wa kuwawezesha wahitimu wa programu hiyo vifaa vya kufanyia kazi ili waweze kujiajiri.

Naye Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhandisi Cyprian Luhemeja, amesema programu ya ukuzaji ujuzi kwa njia ya uanagenzi imelenga kuwezesha nguvukazi ya Taifa, hususani iliyopo katika soko la ajira, kupata ujuzi na stadi za kazi stahiki ili iweze kujiajiiri au kuajiriwa.

Amesema jumla ya shilingi bilioni 2.7 zimetengwa ili kuwezesha utekelezaji wa programu kwa vijana 6000 wakiwemo wenye ulemavu 84.

Katika chuo cha VETA Mwanza jumla ya wanafunzi 132 (wanaume 102 na wanawake 30) wanaendelea na mafunzo katika fani za Useremala, Uashi, Upakaji rangi, Ufundi Mashine za kuchakata Pamba, Ufundi Bomba, Umeme wa Majumbani, Ufundi Magari, Upishi na Uchomeleaji na Uungaji Vyuma.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), CPA Antony Kasore, VETA imeanzisha programu mbalimbali ambazo zinawasaidia wananchi wa Kitanzania kupata ujuzi na kufanya shughuli mbalimbali ambazo zitawaingizia kipato.

Baadhi ya vijana wanaopata mafunzo hayo, wameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan, kwa kuwapatia fursa hiyo muhimu na kusema baada ya mafunzo hayo wanatarajia kujiajiri ili kuweza kujikimu katika maisha yao.

Aidha, wanafunzi hao wameiomba Serikali kuwasaidia vifaa vya kazi za ufundi stadi kwa fani mbalimbali walizojifunza ili utekelezaji wa shughuli hizo baada ya kuhitimu uweze kufanikiwa.



No comments:

Post a Comment