CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Friday 31 May 2024

PROF. MCHOME AIAGIZA VETA KUZIFIKISHA KAZI ZA UBUNIFU KWENYE SOKO

 

Mwenyekiti wa Bodi ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Prof. Sifuni Mchome, ameiagiza Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kuongeza kasi ya uzalishaji wa bidhaa mbalimbali za kiubunifu ili kutatua changamoto za wananchi na kuzalisha kipato.

Prof. Mchome ametoa maagizo hayo tarehe 30 Mei, 2024 jijini Tanga alipotembelea banda la VETA kwenye Maadhimisho ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayofanyika jijini humo.

Amesema walimu na wanafunzi wa vyuo vya VETA nchini wanafanya kazi nyingi za kiubunifu ambazo zinahitajika kwa wingi katika kuongeza ufanisi kwenye shughuli za uzalishaji zinazofanywa na wananchi lakini bidhaa hizo za kiubunifu hazijaweza kuzalishwa kwa wingi na kuwafikia wahitaji.

“Kwa kweli nimeridhika sana na ubunifu unaofanyika na vitu mbalimbali vinavyozalishwa kupitia VETA … sehemu zote nilizopita unaona ni vitu vinavyoenda kusuluhisha changamoto mbalimbali za watanzania lakini changamoto ni kuvizalisha kwa wingi ili vifike sokoni,”amesema.

Prof Mchome amesema ni wajibu wa VETA kutoa mafunzo ya ufundi stadi na kuwajengea ujuzi Watanzania pamoja na kutumia wabunifu wake kuzalisha bidhaa zitakozowawezesha kujipatia kipato kuanzia kwa mwanafunzi, mwalimu na taasisi kwa ujumla.

“Ujumbe wangu ambao nimekuwa nikiutoa sehemu zote ni kuwa tutengeneze pesa kwa kuwa kazi ya ujuzi ni kazi ya kuzalisha vitu vinavyohitajika kwenye soko la kitaifa na kimataifa na kufanya biashara kupitia vitu hivyo,” amesema

Prof. Mchome amewahamasisha wanafunzi na walimu wa VETA kuwa na mtazamo wa biashara ili wanapobuni vitu mbalimbali waweke msukumo katika kuvizalisha kwa wingi.

Kwa mujibu wa Prof. Mchome, mtazamo wa kibiashara utawezesha wahitimu wa VETA kujikita katika kuanzisha makampuni na kuzalisha bidhaa mbalimbali kutokana na mafunzo na fikra za kibiashara walizojengewa tangu wanapojiunga na vyuo vya VETA.




No comments:

Post a Comment