Wanafunzi kutoka vyuo
mbalimbali vya VETA wametawala Mashindano ya Kitaifa ya Ujuzi mwaka huu ambapo
wameibuka washindi kwa nafasi za kwanza hadi tatu katika mashindano hayo
yaliyofanyika tarehe 30 na 31 Mei, 2024, jijini Tanga.
Mashindano hayo
yaliyofanyika katika viwanja vya shule ya sekondari Popatlal yalihusisha wanafunzi 25 kutoka vyuo
mbalimbali vya ufundi stadi katika fani za ufundi Uashi, Ufundi Umeme,
Mekatroniki, Sanaa ya Mapishi pamoja na Uungaji na Uundaji vyuma.
Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb)
amewakabidhi zawadi za ushindi washindi hao, tarehe 31 Mei, 2024, wakati wa
kilele cha Maadhimisho ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu.
Mwanafunzi Ibrahimu
Simba kutoka chuo cha VETA Kihonda ameibuka mshindi wa kwanza katika fani ya
Uashi na kufuatiwa na Ramadhani Hussein wa chuo cha VETA Tanga na wa tatu ni
Shaban Hamdani wa chuo cha VETA Tanga.
Katika fani ya Ufundi
Umeme, Omari Hussein wa Chuo cha VETA Kihonda ameibuka mshindi wa kwanza
akifuatiwa na Silvester Mngo'ngo wa chuo cha Almakhtoum College of Engineering
na wa tatu ni Goodluck Justine wa chuo cha VETA Kipawa.
Mfungo Sebastian wa
chuo cha VETA Kipawa ameibuka mshindi wa
kwanza kwenye fani ya Mekatroniki na kufuatiwa na Godwin Justine wa chuo cha VETA Dodoma na wa tatu ni Ester Fabian
wa chuo cha VETA Kipawa.
Katika fani ya Uungaji na Uundaji Vyuma, Ramadhani Rajabu wa Chuo cha VETA Tanga ameibuka mshindi wa kwanza akifuatiwa na Ivon Ngonyani wa chuo cha VETA Mikumi na wa tatu ni Jonas Makongo wa chuo cha VETA Tanga.
Hamisa Rashidi kutoka
chuo cha VETA cha Hoteli na Utalii ameibuka mshindi wa kwanza kwenye fani Sanaa
ya Mapishi na kufuatiwa na Prudence Kirori wa chuo cha VETA cha Hoteli na
Utalii na wa tatu ni Haruna Jumanne kutoka
Chuo cha Uhasibu Arusha.
Washindi wa kwanza
wamekabidhiwa zawadi ya fedha taslimu kiasi cha Tshs Milioni moja , washindi wa
pili shilingi laki nne na wa tatu kiasi cha shilingi laki mbili.
Mashindano hayo ni
miongoni mwa shughuli zilizokuwa zikifanyika katika Maadhimisho ya Kitaifa ya
Elimu, Ujuzi na Ubunifu yaliyoanza tarehe 25 Mei, 2024, ambapo kilele chake
kilikuwa tarehe 31 Mei, 2024.
No comments:
Post a Comment