CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Wednesday, 16 August 2017

VETA, Airtel wazindua namba za huduma kwa wateja wa VSOMO



Mamlaka ya Elimu na mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kwa kushirikiana na kampuni ya simu za mkononi Airtel kupitia programu ya utoaji wa mafunzo ya ufundi stadi kwa njia ya simu (VSOMO) wamezindua namba maalum kwa ajili ya kuwahudumia wananchi kwa karibu zaidi.

Mgeni rasmi katika uzinduzi huo, Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Dar es Salaam Habibu Bukko amesema kupitia namba 0699859573 na 0699859572 wananchi watapata maelekezo yote muhimu yanayohusiana na VSOMO.

Amesema lengo la VETA ni kuendelea kuwawezesha watanzania kushiriki kikamilifu katika sera ya uchumi wa viwanda kwa kuhakikisha wanapata ujuzi popote pale wanapokuwa.
“Wananchi wanaweza kupiga simu namba 0699859573 na 0699859572 kila siku kuanzia saa 2 asubuhi hadi saa 10 jioni na kuuliza maswali, ufafanuzi na kutoa mapendekezo juu ya programu ya VSOMO na kupata majibu papo kwa hapo”Alisema

Mkuu wa Chuo cha VETA Kipawa ambaye pia ni mratibu wa VSOMO Eng. Lucius Luteganya amesema mwitikio wa wananchi na hasa vijana katika programu hiyo ni wa kuridhisha na kwamba takwimu zinaonyesha zaidi ya vijana 30,000 tayari wamepakua application ya VSOMO, 8000 wamejiandikisha na kati yao 50 wanasoma kozi mbalimbali na wengine tayari wameshahitimu na kupata vyeti vya VETA.


“Tumeona kuna umuhimu wa kuweka namba hizi maalum ili kuweza kuwahudumia wananchi kwa karibu zaidi hasa katika kipindi hiki ambacho mpango huu wa VSOMO unazidi kupanuka kwa kuongeza kozi nyingi kulingana na mahitaji” Alisema

Alizitaja kozi zinazopatikana kwa njia ya VSOMO kwa sasa ni Huduma ya chakula na mbinu za kuhudumia wateja, Matengenezo ya Kompyuta, Umeme wa viwandani, Ufundi Bomba wa Majumbani,  Umeme wa magari, Ufundi umeme wa majumbani, Ufundi pikipiki, Ufundi wa simu za mkononi, Ufundi Alluminium, Utaalamu wa maswala ya urembo pamoja na Ufundi wa kuchomea vyuma.

Meneja Uhusiano wa Airtel Jackson Mbando alisema kampuni yake inajisikia fahari kuendelea kuongeza ubunifu katika programu ya VSOMO na lengo ni kuboresha na kurahisisha upatikanaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi.


Alisema kila simu itakayopigwa itachajiwa gharama ya shilingi 60 tu na kwamba mteja hatapangiwa muda wa kuongea na mtoa huduma hadi mwisho wa kuhudumiwa.

Programu ya utoaji wa mafunzo kwa njia ya simu (VSOMO) ilizinduliwa mwezi June 2016 ambapo wananchi wanaweza kupakua application hiyo kutoka kwenye Google Play Store na kujisajili na kuanza masomo kwa njia simu na wakifaulu huchagua chuo wanachopenda kuhudhuria mafunzo ya vitendo na wakifaulu hutunukiwa vyeti vya VETA.


No comments:

Post a Comment