CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday, 17 August 2017

VETA na Ujerumani zatiliana saini makubaliano ya mafunzo ya uwanagenzi katika teknolojia ya ufundi wa zana za kilimo na mitambo ya ujenzi



Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imetiliana saini makubaliano yenye thamani ya Euro 900,000 (zaidi ya shilingi bilioni 2.3) na Chemba ya Baraza la Ufundi Stadi ya Ujerumani (WHKT) kwa ajili ya mafunzo ya uwanagenzi yenye lengo la kuimarisha ufundi wa zana za kilimo na teknolojia ya mitambo ya ujenzi.

Makubaliano hayo yalitiwa saini Alhamisi, 17 Agosti, 2017 na Moshi Kabengwe, Mkurugenzi wa Utawana na Usimamizi wa Rasilimali watu, aliyemwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dk Leonard Akwilapo kwa upande wa Tanzania na Mtendaji Mkuu wa WHKT, Bw. Reiner Nolte kwa upande wa Ujerumani.  

Utiaji saini makubaliano hayo ulishuhudiwa na Barozi wa Ujerumani nchini, Dk. Detlef Waechter, Mwenyekiti wa Board ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi Bw. Peter Maduki, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Dk. Bwire Ndazi na Maafisa wengine waandamizi wengine wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, VETA na Ujerumani.

Waraka wa makubaliano hayo unaeleza kuwa utekelezaji wa mradi utaanza mara baada ya kusaini hadi tarehe 31 Machi, 2020, lakini kuna fursa ya kuongeza muda zaidi kutegemeana na uzoefu kutoka katika mradi wa awali na makubaliano ya pande zote mbili.

“ujuzi wa mafundi na wakulima utaboreshwa kupitia kozi zitakazotolewa na VETA kwa mfumo wa uwanagenzi. Kozi hizo ni pamoja ufundi zana za kilimo, ufundi mitambo ya ujenzi na mafunzo ya vitendo katika teknolojia ya kupunguza upotevu wa mavuno ya mazao ya kilimo katika maeneo yatakayoainishwa,” inaeleza sehemu ya waraka wa makubaliano.

Utekelezaji wa  mradi huo unakuja baada ya kupata uzoefu wa ushirikiano katika mradi mwingine kati ya VETA na Chemba ya Ufundi Stadi ya Ujerumani kwenye mafunzo kwa njia ya uwanagenzi katika fani za ufundi magari, ufundi umeme na huduma za hoteli ambao umekuwa ukitekelezwa tangu mwaka 2011 hadi sasa. Uwanagenzi ni mfumo unaohusisha mafunzo yanayohusisha ngwe za mzunguko kati ya chuo cha ufundi na sehemu ya kazi.

Akizungumza wakati wa kusaini makubaliano hayo, Balozi wa Ujerumani nchini Dk. Detlef Waechter alisema anatarajia kuwa ushirikiano katika mradi huo utawasaidia kwa kiasi kikubwa Watanzania wengi, hususani vijana katika kupata ujuzi wa kuutumia katika kuongeza tija kwenye kilimo nchini.

Alisema, Ujerumani ina uzoefu mkubwa na wa muda mrefu katika utoaji mafunzo  kwa njia ya uwanagenzi na kwa hivyo Tanzania ina mengi ya kujifunza kutoka Ujerumani.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimani watu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknoloji Bw. Moshi Kabengwe aliishukuru serikali ya Ujerumani kwa msaada na ushirikiano na kusema kuwa utawasaidia vijana wengi kuajirika na kuwa na ujuzi wa kutumia teknolojia za kisasa katika kilimo.

Naye Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dk. Bwire Ndazi aliishukuru serikali ya Ujerumani kwa kuendelea kuiamini VETA na kuendeleza ushirikiano nayo katika utoaji mafunzo kwa mfumo wa uwanagenzi.

Alisema, ushirikiano katika miradi ya nyuma umeendelea kuwanufaisha vijana wengi kupata ujuzi na kuweza kuajirika kwa urahisi.

Mafunzo ya uwanagenzi huendeshwa kwa mfumo wa ngwe za mzunguko kati ya chuo cha ufundi stadi na sehemu ya kazi ambapo  mwanafunzi hupata mafunzo ya ujuzi kwenye karakana za chuo na uzoefu wa hali halisi mahala pa kazi, hivyo kumwongezea umahiri pamoja na maarifa zaidi na utamaduni wa ya mazingira ya kazi husika.


No comments:

Post a Comment