CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Tuesday 15 December 2020

Wahitimu VETA waaswa kujituma

Wahitimu wa Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi na Huduma Dar es Salaam wametakiwa kuendeleza bidii na moyo wa kujituma waliojengewa wakati wa masomo katika sehemu zao za kazi ili waweze kufanikiwa.

Akizungumza katika mahafali ya 50 ya Chuo hicho iliyofanyika tarehe 4 Desemba, 2020 jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke, Ndugu Deogratius Lukomanya aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya hiyo Mhe. Godwin Gondwe, alisema ili kijana aweze kufanikiwa akiwa kazini ni lazima kuweka bidii na hamasa ya kujituma katika kazi zozote atazokuwa anazifanya.

Lukomanya amewataka wahitimu hao kuondokana na dhana ya kusubiria kuajiriwa bali wajitume kwa kujitengenezea ajira wao wenyewe ili waweze kutoa ajira kwa vijana wengine.

“Katika karne hii ya ishirini na moja, upatikanaji wa ajira umekuwa ni changamoto kubwa ulimwenguni kote, hivyo ni wajibu wenu kuwa na mawazo ya kujitengenezea ajira zenu wenyewe kwa ujuzi mliopata,” alisema.

Ndugu Lukomanya aliwataka waajiri kuendelea kuwapokea wanafunzi na wahitimu wa VETA katika viwanda na makampuni yao na kuwapa nafasi za mafunzo kwa vitendo pamoja na ajira pale zinapopatikana.

Mkuu wa Chuo cha VETA Dar es Salaam, Bw. Joseph Mwanda, alisema kwa mwaka 2020, jumla ya vijana 616 wamehitimu masomo yao katika kozi za ufundi stadi katika ngazi ya pili (Level II), ngazi ya tatu (Level III) na ngazi ya Diploma.

Alisema chuo hicho kimeweza kusajili jumla ya wanafunzi 1,361 kwa kozi za muda mrefu na 10,808 kwa kozi za muda mfupi kwa kipindi cha kuanzia Julai 2019 hadi Oktoba 2020.

Kwa mujibu wa Ndugu Mwanda, chuo hicho kimekuwa kikitoa mafunzo ya ufundi stadi kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum ambapo kwa mwaka 2020 jumla ya wanafunzi 21 wenye mahitaji maalum wamesajiliwa katika fani za uungaji vyuma na ushonaji.

"Kati ya wanafunzi tuliowasajiliwa wenye mahitaji maalum, kumi ni wenye ulemavu wa mfumo wa akili na wengine kumi na moja wana ulemavu wa viungo ambapo wengi wao wameonyesha uwezo mkubwa kwenye masomo yao,”alisema.

Mwanda alisema vijana hao wamekuwa wakionyesha uwezo mkubwa kwenye masomo yao huku akitoa mfano wa mhitimu Neema Eliasi Chole wa fani ya ushonaji ambaye amekuwa akifanya vizuri katika masomo yake na kupata wastani wa alama ‘B’ katika  mtihani wa Taifa na hatimaye chuo kuamua kumzawadia Cherehani kwa kutambua jitihada zake na kumwezesha kujiajiri.

Akizungumza kwa niaba ya wazazi waliohudhuria mahafali hayo, Bi. Aveline Mrema amewahimiza wahitimu kutokata tamaa  katika maisha yao kwani ukarasa mpya wa maisha umeanza ambapo wahitimu hao  wanaweza kukumbana na changamoto mbalimbali wanapoingia kwenye soko la ajira. 

Naye mwakilishi wa waajiri kutoka kampuni ya Reveurse Tanzania Limited, Bi. Njile Bwana, alipongeza VETA kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kukuza ujuzi kwa vijana ambapo alisema kupitia kampuni yake inayoshughulika na ajira, kampuni nne zimeonesha nia ya kuchukua wahitimu wa VETA hali inayoonyesha ni kwa namna gani vijana wa VETA ni bora.



No comments:

Post a Comment