CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Friday 1 October 2021

JUMBE HARUNI, MHITIMU WA VETA ALIYEANZISHA KAMPUNI NA KUAJIRI VIJANA WENZAKE

 


Jumbe Haruni Jumbe ni mhitimu wa VETA katika fani ya Ufundi Bomba kutoka Chuo cha Ufundi Stadi na Huduma Kihonda. Alihitimu mwaka 1997 na kuamua kujiajiri..

“Ilikuwa mwaka 1998 ambapo wazazi wangu waliniwezesha vifaa vya kufanyia kazi nikaingia mtaani kufanya kazi za ufundi bomba na uchomeleaji na hatimaye nikaweza kuanzisha kijiwe changu maeneo ya nyumbani kwetu Mzumbe mkoani Morogoro” Anasema.

Anasema mwaka 2003 alihama kutoka Mzumbe na kuelekea Mikumi, Morogoro  ambako aliendelea na shughuli hizo za ufundi kwa kufungua karakana rasmi. Mafanikio aliyoyapata kupitia karakana yake, yalimwezesha kufungua kampuni yake ya Jumbe Plumbers and General Maintenance na kuisajili rasmi mwezi Septemba 2007.

“Juhudi, maarifa, uaminifu na kuipenda kazi yako kwa kuifanya kwa wakati na kama alivyokubaliana na wateja wako, ndo kunakokuchangia kwa kiasi kikubwa kukufanya upate wateja wengi, kujulikana  na kudumu katika biashara yako,” anasema.

 Licha ya kupata mafanikio katika shughuli zake, Jumbe anasema katika karakana  yake amesaidia vijana wengi kujifunza ufundi na hata  kuajiri wengine. Kwa sasa ameajiri vijana wanne.

“Nilipokea vijana wa aina mbalimbali na kuwafunza ufundi bomba na kuchomelea vyuma... Vijana hawa walipenda kujifunza lakini wazazi wao hawakuwa na uwezo kuwapeleka VETA,” Anasema.

Pamoja na ujuzi na uzoefu katika kazi za Ufundi Bomba, Jumbe alifanikiwa kubuni mifumo mbalimbali ya kuwezesha upatikanaji wa maji moto kwa kutumia nishati ya jua, ubunifu ambao umemwezesha kushinda katika Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) mwaka 2019. 

Hata hivyo Jumbe anasema hajaweza kupata fursa pana ya kujitangaza ili kupata soko la bidhaa za kibunifu kufikia watu wengi zaidi ndani  na nje ya nchi.

Jumbe anawashauri vijana nchini kujiunga na mafunzo ya Ufundi Stadi kwani yatawawezesha kuajiriwa au kujiajiri wao wenyewe na vijana wenzao.




No comments:

Post a Comment