Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi iko katika hatua za mwisho kukamilisha maandalizi kwa ajili ya utoaji mafunzo ya Uvuvi katika ngazi ya ufundi stadi.
VETA
imeshanunua zana na vifaa mbalimbali kwa ajili ya mafunzo hayo, ikiwemo boti
(MV VETA 01) ambayo tarehe 9 Oktoba ilipokelewa na kupelekwa kwenye Chuo cha
Ufundi Stadi cha Wilaya ya Chato ambacho ndio kitakuwa chuo cha VETA cha kwanza
kutoa mafunzo hayo.
Tarehe 25 Mei 2021 VETA ilipokea vifaa mbalimbali vyenye thamani ya Yuan
milioni moja karibu sawa na shilingi milioni 350 kwa ajili ya kufundishia fani
ya Uvuvi na Uchakataji wa Samaki vilivyonunuliwa kwa msaada wa Serikali ya
Jamhuri ya Watu wa China.
Hafla ya makabidhiano ya vifaa hivyo ilifanyika kwenye ofisi za yalipokuwa
Makao Makuu ya VETA jijini Dar es Salaam na kuwahusisha Mheshimiwa Prof. Joyce
Ndalichako, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia na Mheshimiwa Wang Ke,
Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania.
Vifaa hivyo vilitokana na ahadi ya Mheshimiwa Wang Yi, Waziri wa Mambo
ya Nje wa China na Mjumbe wa Baraza la Taifa la nchi aliyoitoa tarehe 7 Januari
2021 wakati wa Uzinduzi wa Chuo cha Ufundi Stadi cha Wilaya ya Chato. Kwa niaba
ya Serikali yake, Mheshimiwa Yi aliahidi kutoa kiasi cha Yuan milioni moja
karibu sawa na shilingi milioni 350 kwa ajili ya kununua vifaa vya Mafunzo ya
Stadi za Uvuvi na Uchakataji Samaki kwa ajili ya Chuo cha Ufundi Stadi cha
Wilaya ya Chato.
Katika hafla hiyo, Prof. Ndalichako alisema kuwa ingawa vipo vyuo
vinavyotoa mafunzo yanayohusiana na Uvuvi na Uchakataji Samaki katika ngazi za
juu, hakukuwa na chuo kinachotoa mafunzo ya namna hiyo kwenye ngazi ya ufundi
stadi.
Alisema kuanzishwa kwa mafunzo hayo kunatarajiwa kuwasaidia kwa kiasi
kikubwa wananchi wa mikoa inayozunguka Ziwa Victoria kuboresha shughuli zao za
kiuchumi ambazo zinahusiana na uvuvi na biashara ya samaki.
“Miongoni mwa manufaa yanayotarajiwa ni kuongeza mavuno ya samaki na
kuongeza thamani ya samaki na mazao yake,” amesema.
Aliiagiza VETA kuendelea kupanua mafunzo hayo katika vyuo vingine, hasa
vinavyozunguka maziwa, bahari na mito mikubwa ambako shughuli kubwa za wananchi
wa mikoa hiyo ni uvuvi na biashara ya samaki.
Naye Naye Balozi wa China nchini, Wang Ke, amesema Serikali yake
itaendelea kusaidia miradi mbalimbali ya elimu nchini kwani inatambua kuwa
elimu ina mchango mkubwa sana katika kuongeza tija na kuchangia maendeleo ya
taifa.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu amesema
VETA itaendelea kupanua mafunzo hayo katika vyuo vingine hatua kwa hatua.
“Tunafungua ukurasa mpya Chato. Kama nasaha za Waziri zilivyotuasa, ni
wakati wa kujipanga vyuo vilivyo katika maeneo ya wavuvi, hasa vinavyojengwa
sasa, kama Mafia, Ukerewe, Kagera, Rufiji, Pangani, Nyasa, Uvinza, n.k. Na
vikongwe pia kama Mwanza, Mara na Dar es Salam,” amesema.
Viongozi na watendaji wengine waliohudhuria hafla hiyo ni pamoja na Dkt.
Leonard Akwilapo, Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia; Dkt.
Ethel Kasembe, Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Elimu ya Ufundi, Wizara ya
Elimu, Sayansi na Teknolojia; Ndugu Peter Maduki, Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa
ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi; Wakurugenzi na Menejimenti ya Makao Makuu
pamoja na Wakuu wa vyuo vya VETA vya Chato, Kipawa na Dar es Salaam. Mkurugenzi
Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu ndiye aliyekuwa mwenyeji wa tukio hilo.
No comments:
Post a Comment