Kampuni
ya Uchimbaji Dhahabu ya Geita (Geita Gold Mine - GGM) imeipatia Mamlaka ya
Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) vifaa vyenye thamani ya Shilingi za
Kitanzania milioni 132 kwa ajili ya kuendesha mafunzo ya ufundi stadi katika
Chuo cha Ufundi Stadi na Huduma cha Mkoa wa Kilimanjaro (VETA Moshi).
Hafla
ya makabidhiano ya vifaa hivyo imefanyika leo, tarehe 26 Oktoba 2021, katika
Chuo cha VETA Moshi, ambapo Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe. Stephen Kagaigai,
alikuwa Mgeni Rasmi na amevipokea kwa niaba ya Serikali na kuvikabidhi kwa
Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu, kwa ajili ya usimamizi wa
matumizi yake. Katika makabidhiano hayo, Kampuni ya GGM iliwakilishwa na Makamu
wa Rais wa Kampuni hiyo, Bw. Simon Shayo.
Vifaa
hivyo vimelenga kuboresha mafunzo ya Uanagenzi yanayoendeshwa kwa ushirikiano
kati ya VETA na Umoja wa Wachimba Madini nchini (TCM) kupitia mradi wa Mafunzo
Maalum ya Ufundi kwa ajili ya Sekta ya Madini, maarufu kwa jina la IMTT.
Akizungumza
wakati wa hafla hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mh. Stephen Kagaigai,
ameushukuru GGM kwa msaada huo wa vifaa na kueleza kuwa matumaini yake ni kuwa
vifaa hivyo vitakwenda kuleta mabadiliko makubwa katika karakana za chuo cha
VETA Moshi na kuwasaidia wanafunzi kujifunza kwa vitendo zaidi na kuhitimu
wakiwa na ujuzi na umahiri wa viwango vya kimataifa. Aliwaomba wadau wengine wa
Ufundi Stadi kuiga mfano huo wa GGM na kuunga mkono kwa vitendo juhudi za
Serikali ya Awamu ya Sita za kuimarisha Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi
nchini.
“Nitumie
fursa hii pia kuwaomba wanachama wengine wa TCM kuunga mkono juhudi za Serikali
ya Awamu ya Sita, za kuzalisha mafundi stadi mahiri kwa ajili ya viwanda vyetu.
Ufundi stadi ndio msingi mkubwa wa maendeleo ya viwanda. Kwa hiyo, tukiimarisha
elimu na mafunzo ya ufundi stadi tutaleta matokeo makubwa kiuchumi; na hili ni
jukumu letu sote," alisema.
Amewashauri
VETA na TCM kueneza mpango huo wa mafunzo kwa njia ya uanagenzi kwenye vyuo
vingine vya VETA na kuanzisha miradi mingine inayofanana na huo ili manufaa
yaliyopatikana kupitia chuo cha VETA Moshi yaweze kuenea nchi nzima na kuwanufaisha
vijana wengi zaidi.
Kwa
upande wake, Makamu wa Rais wa Kampuni ya GGM, Bw. Simon Shayo, ameiomba
Serikali kuhakikisha fedha za Tozo ya Uendelezaji Ujuzi (Skills Development
Levy - SDL) inayopelekwa kwenye Ofisi Waziri Mkuu itumike zaidi kuboresha
mafunzo ya ufundi stadi na mengine yanayofanana na hayo ili kupanua wigo wa
uendelezaji ujuzi.
Mkurugenzi
Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu alishukuru kampuni ya GGM kwa kuwa mfano wa
kipekee katika kuthamini na kuchangia juhudi za uendelezaji ujuzi.
Amesema
tangu kuanzishwa kwa mradi wa IMTT, kampuni za GGM na Bulyanhulu Gold Mine
Limited zimekuwa mfano wa kuigwa kwa kujitoa kwa hali na mali katika kufadhili
uanzishwaji na uendelezaji wa mradi huu.
“Kampuni
hizi mbili ndizo zilizotoa fedha kwa ajili ya ukarabati wa karakana, ununuzi wa
mitambo na zana mbalimbali za mafunzo, pamoja na kugharimia mafunzo maalum ya
walimu yaliyofanyika nchini Afrika ya Kusini. Hata baada ya mradi kuanza wao
ndiyo wamekuwa kinara katika kutoa ufadhili kwa wanafunzi wa uanagenzi waliosoma
kupitia mradi huu,” amesema.
Naye
Katibu Mtendaji wa TCM, Bw. Gerald Mturi, ameishauri Serikali kuanzisha chombo
kinachofanana na Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) ambacho kitakuwa na majukumu
ya kukusanya na kusimamia Tozo ya Uendelezaji Ujuzi (Skills Development
Levy-SDL) na kuigawa kwenye taasisi mbalimbali kulingana na mahitaji halisi na
kwa ajili ya matumizi sahihi.
No comments:
Post a Comment