Jumla
ya vijana 200 jijini Dar es Salaam wanatarajia kunufaika na mafunzo maalum ya
ufundi stadi kwenye sekta ya ujenzi kupitia programu ya 2jiajiri inayofadhiliwa
na Benki ya KCB Tanzania.
Akizungumza
wakati wa utiaji saini makubaliano ya utekelezaji wa mpango huo kati ya Benki
ya KCB Tanzania na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) tarehe 7
Oktoba, 2021, Meneja Mawasiliano na Uhusiano wa Benki hiyo, Margaret Mhina,
amesema lengo la programu hiyo ni kuwezesha vijana kujipatia ujuzi ili kuweza kujiajiri
mara tu wanapohitimu.
“Tunalenga
kumtoa kijana kwenye fikra za kuajiriwa na kumpeleka kwenye mawazo ya kujiajiri
na kuajiri vijana wengine… Tunaamini kabisa kuwa VETA ni sehemu sahihi ya
kuwezesha vijana kujiajiri kwa kupitia mafunzo wanayoyatoa,” Amesema.
Kwa
upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu, ameishukuru Benki ya
KCB kwa kutoa sehemu ya faida yao kufadhili vijana kujipatia mafunzo ya ufundi
stadi kupitia chuo cha VETA Dar es Salaam, na kuongeza kuwa anaamini mafunzo
hayo yatawezesha vijana hao kujitegemea, kuboresha maisha yao na hatimaye
kukuza uchumi wa nchi.
“Tunawapongeza
sana KCB kutokana na ukweli kwamba wameamua kuwekeza sehemu sahihi ambayo
italeta matokeo endelevu na kuongeza chachu ya ukuaji wa uchumi. Vijana
watakaopata mafunzo haya hawatakuwa tegemezi tena," Amesema.
Dkt.
Bujulu amesema VETA itahakikisha kuwa mafunzo hayo yanatolewa kwa ufanisi ili
hatimaye vijana hao wapate ujuzi stahiki utakaowawezesha kulitumikia Taifa kwa
umahiri.
Mkuu wa Chuo cha VETA Dar es Salaam, Joseph Mwanda, amesema mafunzo hayo yatatolewa kwa miezi mitatu kuanzia mwezi Oktoba, 2021 hadi Januari, 2022 katika fani za Uashi (Masonry & Brick laying), Umeme wa Majumbani (Electrical Installation), Ufundi Bomba (Plumbing & Pipe Fitting), Ufundi wa Aluminiam (Aluminium Works) na Usanifu na Upakaji Rangi (Painting & Sign Writing).
No comments:
Post a Comment