CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Tuesday 26 October 2021

Wadau wapongeza uandaaji wa mitaala bora ya Ufundi Stadi kwenye Kilimo na Ufugaji

 

Wadau wa Sekta za Kilimo na Mifugo wameipongeza Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kwa kuandaa mitaala yenye mchanganuo mzuri wa stadi muhimu kwa ajili ya utoaji mafunzo ya ufundi stadi kwenye sekta hizo.

Tarehe 21 Oktoba 2021, VETA kwa kushirikiana na Shirika la Kimataifa Care iliratibu kikao cha wadau wa Sekta za Kilimo na Mifugo kwa ajili ya kupitia na kutoa maoni yao kwenye miswada ya Mitaala na Mafunzo ya Ufundi Stadi katika fani za Kilimo cha Mazao ya Shamba (Field Crop Production) na Mazao ya Bustani (Horticultural Crop Production) na uhuishaji wa Mtaala wa fani ya Ufugaji wa Wanyama (Animal Husbandry).

Wadau hao waliokutana na kupitia miswada hiyo katika hoteli ya Flomi, mjini Morogoro walitoa pongezi nyingi kwa VETA kwa hatua hiyo wakieleza kuwa sekta hizo ni tegemeo kubwa kwa maisha ya Watanzania wengi na kwamba iwapo mitaala hiyo itatekelezwa ipasavyo, itasaidia vijana wengi kupata ujuzi utakaowawezesha kuleta mabadiliko makubwa katika sekta ya kilimo.

Fabian Mwakatuma, Mwenyekiti Baraza la Ujuzi la Kilimo, kutoka Mfuko wa Sekta Binafsi (TPSF) alisema kuna uhaba mkubwa wa watu wenye stadi katika maeneo ya kilimo na ufugaji huku kukiwa na fursa nyingi.

Aliongeza kuwa mbali na ukweli kuwa zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania wanategemea kilimo katika kuendesha maisha yao, kuna fursa nyingi za kunufaika na usindikaji wa mazao mbalimbali ya kilimo na mifugo iwapo watu watapata stadi katika maeneo hayo.  

Kaimu Mkurugenzi wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Stella Ndimubenya amesema VETA sasa inaweka mipango na kufanya jitihada mbalimbali zinazolenga kupanua utoaji wa mafunzo ya ufundi stadi katika sekta za Kilimo na Mifugo kwa kutambua umuhimu wake katika jamii na uhitaji wa stadi kwenye sekta hizo. 

Baada ya kukamilisha mitaala hii na kupitishwa na Bodi, tutaanza ku-package (kuandaa) kozi mbalimbali zinazohusiana na kilimo na mifugo kulingana na mahitaji.

Naye Meneja Mradi wa Tajirika na Kilimo, kutoka shirika la Care alisema, wakati wa utekelezaji mradi huo kwa kushirikiana na VETA walibaini uhitaji mkubwa wa mafunzo ya ufundi stadi katika jamii za wakulima.



No comments:

Post a Comment