Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Mhe. Profesa Joyce Ndalichako (Mb), ametembelea vyuo vya VETA mkoani Kigoma na kuonesha kuridhishwa na utoaji mafunzo ya uanagenzi kwa vijana yanayoendeshwa na vyuo mbalimbali vya VETA kwa ufadhili wa Ofisi ya Waziri Mkuu.
"Nimeona ndani ya miezi
miwili mambo ambayo mmeshajifunza ni mambo makubwa sana mtafikiri mnamaliza
kesho wakati bado mpo miezi minne, mkimaliza hii miezi minne iliyosalia mtakuwa
mko vizuri zaidi, nawapongeza sana. Natoa pongezi zangu kwa wakufunzi wanaotoa
mafunzo haya, ukiona vyaelea vimeundwa…Haya mazuri ninayoona kwenu vijana ni
kutokana na kazi nzuri inayofanywa na wakufunzi wa VETA...endeleeni kuwapika
vijana wetu…hongereni sana," amesema.
Vilevile, Waziri Ndalichako ametumia fursa hiyo kuzitaka halmashauri nchini kutoa
kipaumbele kwa vijana wanaohitimu mafunzo ya ufundi stadi chini ya mradi huo wakati
wa kutoa mikopo kupitia asilimia kumi ya mapato ya halmashauri ili waweze kuanzisha
shughuli zao na kujiajiri, hivyo kusaidia kutatua changamoto za ajira nchini.
Amesema mfuko wa maendeleo ya vijana ambao uko chini ya ofisi ya Waziri Mkuu
pia umeboreshwa ili kuongeza wigo wa kutoa mikopo kwa vijana, ambapo pia
kiwango kimeongezwa kutoka milioni kumi za awali hadi shilingi milioni 50.
Kaimu Mkuu wa Chuo cha VETA Kigoma, Paul Kimenya, amesema kupitia mafunzo hayo ya uanagenzi, chuo kimenufaika kwa kutumia ujuzi wa wanagenzi hao kufanya ukarabati wa baadhi ya miundombinu ya chuo kadiri ya fani walizosomea pamoja na kupata vifaa vya mafunzo katika karakana ambavyo vimesaidia kuboresha mafunzo chuoni hapo.
Jumla ya vijana 7,760 wanaendelea na mafunzo kwa njia ya Uanagenzi katika vyuo 62 vya ufundi stadi nchini, kati yao 3988 wanapata mafunzo hayo kwenye vyuo 30 vya VETA. Mafunzo hayo yalianza mwezi Juni 2022 na yanatarajiwa kumalizika mwezi Desemba, 2022.
Programu
ya Kukuza Ujuzi nchini inalenga kuwezesha nguvukazi ya Taifa kupata ujuzi na
stadi za kazi stahiki ili kumudu ushindani katika soko la ajira ambapo kwa sasa
inatekelezwa kwa awamu ya nne.
No comments:
Post a Comment