CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday 16 November 2023

Mkurugenzi Mkuu wa VETA atembelea Chuo cha TEHAMA VETA Kipawa

Asisitiza ubunifu matumizi ya TEHAMA kutatua changamoto za jamii na kuongeza uzalishaji

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Dkt. Prosper Mgaya ametembelea Chuo cha TEHAMA cha VETA Kipawa kujionea  shughuli za utoaji mafunzo na kuzungumza na wafanyakazi wa chuo hicho.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo leo tarehe 16 Novemba, 2023, jijini Dar es Salaam, Dkt. Mgaya ameagiza Menejimenti na wafanyakazi wa chuo hicho kuongeza ubunifu katika utoaji mafunzo ya TEHAMA na kuhakikisha TEHAMA inatumika kwa ufanisi kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii.

Amesema chuo hicho maalum kwa ajili ya mafunzo ya TEHAMA kinategemewa kuzalisha wahitimu mahiri wenye uwezo wa kutumia ujuzi wao kurahisisha uendeshaji wa shughuli mbalimbali na kutatua changamoto zinazoikabili jamii.

“Msisitizo wangu kwenu ni kuhakikisha mnatoa mafunzo bora, mnafanya ubunifu utakaoweza kutatua changamoto zinazoikabili jamii yetu na kutoa huduma za kitaalamu kwa jamii na kuongeza mapato ya ndani ambayo yatasaidia kupunguza utegemezi wa ruzuku toka serikalini katika kuendesha shughuli za VETA,”amesema

Dkt Mgaya amesema chuo hicho kina fursa kubwa ya kufanya uzalishaji kupitia utoaji wa huduma mbalimbali za TEHAMA kwa jamii inayowazunguka na kuwataka kufanya ubunifu na kutumia vyema fursa hizo ili kujiongezea kipato.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ina mategemeo makubwa sana na VETA katika kuwawezesha wananchi kujipatia ujuzi na kuwataka wafanyakazi kutimiza wajibu wao kikamilifu ili kufanikisha azma hiyo.

Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Dar es Salaam, Ndugu Angelus Ngonyani amemshukuru Dkt. Mgaya kwa kutembelea chuo hicho na kuahidi kusimamia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa ili kuboresha utoaji mafunzo katika chuo hicho.

Akisoma taarifa ya chuo, Mkuu wa Chuo cha VETA Kipawa, Mhandisi Dickson Mkasanga amesema chuo hicho kina jumla ya wanafunzi 144 wanaoendelea na masomo kwa kozi za muda mrefu katika fani za TEHAMA, Elektroniki, Umeme wa Majumbani na Umeme wa Viwandani.

Amesema katika kipindi cha mwezi Julai, 2022 hadi mwezi Novemba, 2023 chuo hicho kimetoa mafunzo mbalimbali  ya muda mfupi kwa wanafunzi 1,890.

Mhandisi Mkasanga amesema chuo hicho kimejipanga vyema kutoa mafunzo kwenye fani ya mekatroniki ili kuendana na kasi ya ukuaji na uendeshaji wa viwanda na kwamba kwa sasa chuo kina vifaa vya kisasa kwa ajili ya kufundishia fani hiyo.

No comments:

Post a Comment