Mwenyekiti wa Bodi ya
Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Prof. Sifuni Ernest Mchome ametoa wito kwa
vijana wanaopata mafunzo kwenye vyuo vya VETA hapa nchini kuweka utaratibu wa
kufanya kazi kwa pamoja kupitia vikundi na kwenda katika sehemu mbalimbali za
nchi kufanya kazi walizofundishwa wakiwa pamoja, kwa kuwa kuna uwezekano wa
kufanya mambo makubwa.
Prof. Mchome ametoa
wito huo juzi, tarehe 8 Machi, 2024, katika chuo cha VETA Wilaya ya Karagwe,
wakati wa kuhitimisha ziara ya Bodi ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi katika
Chuo cha Ufundi Stadi na Huduma cha Mkoa wa Kagera na Chuo cha Ufundi Stadi cha
Wilaya ya Karagwe, mkoani Kagera.
” Umoja ni nguvu na
utengano ni udhaifu, viijana mkijiunga kwa pamoja, uwezekano wa kufanya mambo
makubwa ni mkubwa na uwezekano wa kupata misaada kutoka sehemu mbalimbali, hasa
Serikalini ni mkubwa,” amesema.
Amesema VETA inatoa
fursa kwa vijana kuweza kujifunza ujuzi unaowawezesha kujiajiri wenyewe na pia
kuweza kupata fursa za kuajiriwa na kwamba kuna fursa nyingi ambazo wananchi,
hasa vijana wanaweza kuzitumia kwa ajili ya kupata mafunzo ya aina mbalimbali
yanayogusa maendeleo ya nchi na maisha yao kwa ujumla.
“Tunamshukuru sana Dkt. Samia Suluhu Hassan,
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa juhudi kubwa ambazo ameweka katika
ujenzi wa vyuo vya ufundi stadi hapa nchini, hizi juhudi tutazisimamia na
tutahakikisha yale yote yaliyopangwa yanajitokeza katika ubora wake ili yalete
ufanisi katika Elimu na mafunzo ya Ufundi stadi,” amesema.
Ameongeza kuwa
miongoni mwa kazi kubwa ni ya kuhamasisha vijana kujiunga na mafunzo ya ufundi
stadi, na baada ya kupata mafunzo wawe na utaratibu wa kufanya kazi kwa pamoja
katika vikundi.
Ametumia fursa hiyo
pia kuwahamasisha vijana wanaohitimu vyuo vya elimu ya juu kujiunga na vyuo vya
VETA ili kupata kitu cha ziada kinachoweza kuwasaidia kuajirika kwa urahisi.
Ziara ya Bodi ya
Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi ilikuwa na lengo la kujionea namna vyuo hivyo
vinavyotoa mafunzo na kujifunza mambo mbalimbali yanayohusu mafunzo ya ufundi
stadi katika vyuo vya VETA.
No comments:
Post a Comment