CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Tuesday 9 April 2024

DIRISHA LA USAJILI MAKISATU 2024 LAFUNGULIWA RASMI

 


Dirisha la usajili wa ubunifu kwa ajili ya Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) limefunguliwa   rasmi, tarehe 9 Aprili 2024.

Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda ametangaza kufunguliwa kwa dirisha hilo  alipokuwa akizindua Maadhimisho ya Kitaifa ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu, kwenye ukumbi wa Wizara, DANIDA, Jijini Dodoma.

“Dirisha la usajili wa Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu, yaani MAKISATU, limefunguliwa rasmi leo tarehe 9 april 2024 na litafungwa  tarehe 8 Mei 2024,” amesema.

Amesema MAKISATU yanahusisha ngazi mbalimbali, zikiwemo vyuo vya elimu ya juu, taasisi za utafiti na maendeleo, vyuo vya ufundi na mafunzo ya ufundi na ufundi stadi, shule za msingi, shule za sekondari na wabunifu kutoka mfumo usio rasmi.


“Mtanzania yoyote mwenye ubunifu wake anakaribishwa kushiriki kwani utakaposhiriki unaongeza fursa ya wewe kusaidiwa na Serikali ili uweze kuendeleza ubunifu wako na kuweza kuuingiza katika soko na katika mpango wa biashara,” amesema.

Amesema, washindi 10 kwenye kila kundi watashiriki katika fainali zitakazofanyika kwenye Maadhimisho ya Kitaifa ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu, jijini Tanga, tarehe 25 hadi 31 Mei, 2024.

Sambamba na MAKISATU, Prof. Mkenda amesema kuwa maadhimisho ya Kitaifa ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu mwaka huu yatahusisha pia Mashindano ya Ujuzi (Skills Competition) yatakayofanyika kwa wanafunzi katika ngazi ya vyuo vya elimu ya ufundi na mafunzo ya ufundi stadi.

“Hii ni nyanja mpya, haikuwepo, washindi watano wa kila fani watashiriki katika maadhimisho ya wiki ya elimu kitaifa na washindi wa juu watatangazwa na watapewa zawadi mbalimbali katika kilele cha maadhimisho hayo na wataweza kushiriki katika mashindano ya ujuzi ya kidunia.”


Amesema, Madhimisho ya Kitaifa ya Wiki ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu  mwaka 2024 yatahusisha maonyesho ya bidhaa, ubunifu na teknolojia mbalimbali, mashindano ya kitaifa ya sayansi teknolojia na ubunifu yaani (MAKSATU),mashindano ya ujuzi kwa wanafunzi wa vyuo vya ufundi na ufundi stadi nchini, ,mikutano na midahalo kuhusu elimu ujuzi sayansi teknolojia, ubunifu na mafunzo kwa wabunifu.

Amesema maadhimisho hayo yanatarajiwa kuwa na washiriki kutoka taasisi za umma na binafsi zipatazo 339 na yatatanguliwa na matukio mbalimbali ambayo yatafanyika katika ngazi za mikoa na halmashauri, ikiwemo maonesho ya ubunifu na teknolojia, mikutano na midahalo chini ya uratibu wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) na wadau wengine.

No comments:

Post a Comment