CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Tuesday 9 April 2024

VETA YAANZISHA RASMI UTOAJI MAFUNZO KWA WAFANYAKAZI WA NDANI

Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) inatarajia kuanza rasmi kutoa mafunzo kwa wafanyakazi wa ndani katika vyuo vyake nchini.

Utoaji mafunzo hayo unatarajiwa kuanza mwishoni mwa mwezi Aprili, 2024 baada ya kukamilika kwa mtaala wa mafunzo hayo ulioandaliwa na VETA kwa kushirikiana na shirika lisilo la kiserikali la Community Volunteers for the world (CVM) la nchini Italia, kupitia Mradi wa Kuwajengea Uwezo Wafanyakazi wa Majumbani.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano ya mtaala na mihtasari ya mafunzo hayo jijini Dodoma, leo, tarehe 8 Aprili, 2024, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Antony Kasore amesema mafunzo hayo yataanza kutolewa katika vyuo vya VETA vya Iringa, Dodoma, Mikumi,Tanga, Dar es Salaam na Lindi.

CPA Kasore amesema mafunzo hayo yalianza kwa majaribio katika vyuo vya VETA Mikumi na Dodoma mwezi Januari, 2023 baada ya kuonekana kwa uhitaji wa kuwajengea uwezo wafanyakazi wa majumbani ili watekeleze kazi hizo kwa ufanisi.

Amesema VETA itatumia mtaala huo kuzalisha wafanyakazi wenye ujuzi na vyeti kama ilivyotarajiwa, ambapo itatoa nafasi kwa wafanyakazi hao kufanya kazi kwa kujiamini na ufanisi zaidi na kushukuru CVM kwa ushirikiano walioutoa.

 “Tunaishukuru CVM kwa kushirikiana nasi katika uandaaji wa mtaala huu na tunatarajia kwamba tutashirikiana zaidi, lakini pamoja na ushirikiano huo tunafikiria kuwa na wakala ambaye atakuwa daraja la kuwaunganisha wafanyakazi wa ndani na soko la ajira pindi wamalizapo mafunzo,” alisema.

Naye Afisa Mkuza Mitaala kutoka VETA na mratibu wa mradi huo, Anna Nyoni amesema mafunzo kupitia mtaala huo yatafundishwa katika maeneo makuu matatu ambayo ni utunzaji wa watoto, utunzaji wa wazee na wafanyakazi watakaofanya kazi nje ya nchi.

Amesema mafunzo hayo yanatarajiwa kutolewa kupitia kozi za muda mfupi kuanzia mwezi mmoja hadi miezi sita kutegemeana na uhitaji na aina ya mfanyakazi anaetarajiwa kupata mafunzo hayo.

Pamoja na maandalizi ya mtaala, tayari walimu 12 wamejengewa uwezo wa kuweza kutoa mafunzo katika vyuo hivyo.

Kwa upande wake, Mwakilishi Mkazi wa CVM, Giovanni Bagna amesema, mbali na kusaidia kuandaa mtaala na mihtasari, shirika lake litasaidia kutoa mikopo nafuu kwa wafanyakazi wa ndani watakaoonesha na nia na uhitaji wa kupata mafunzo na baadae kurejesha kwa utaratibu utakaowekwa ili kuwawezesha wafanyakazi wa majumbani wengi zaidi kunufaika na mafunzo hayo.

Kwa upande wake, Mwakilishi Mkazi wa CVM, Giovanni Bagna amesema, mbali na kusaidia kuandaa mtaala na mihtasari, shirika lake litasaidia kutoa mikopo nafuu kwa wafanyakazi wa ndani watakaoonesha na nia na uhitaji wa kupata mafunzo na baadae kurejesha kwa utaratibu utakaowekwa ili kuwawezesha wafanyakazi wa majumbani wengi zaidi kunufaika na mafunzo hayo.



No comments:

Post a Comment