Naibu Katibu Mkuu wa
Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt Franklin Rwezimula, amekitaka Chuo
cha Ualimu wa Ufundi Stadi Morogoro (MVTTC) kupanua wigo wake wa udahili na
kuboresha utoaji wa mafunzo ili kiweze kuwa kituo mahsusi cha kutoa walimu mahiri
na wa kutosha kwa ajili ya vyuo vya ufundi stadi vinavyoendelea kujengwa
nchini, pamoja na wakufunzi wa karakana (workshop instructors) kwa ajili ya
shule za sekondari za amali.
Dkt. Rwezimula ametoa
wito huo wakati wa mahafali ya 26 ya MVTTC, tarehe 22 Machi, 2024,
iliyowahusisha walimu tarajali 218 wa ualimu wa ufundi stadi kwa ngazi ya
Astashahada na Shahada.
Dkt Rwezamula ambaye
alikuwa mgeni rasmi katika mahafali hayo, amesisitiza umuhimu wa Mamlaka ya
Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) katika utekelezaji wa maono ya Serikali
ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.
Samia Suluhu Hassan, ya kuleta mageuzi makubwa katika Sekta ya Elimu kwa
kuhakikisha Watanzania wanapata ujuzi na maarifa yatakayowasaidia kujiajiri na
kukuza uchumi wa Taifa.
Amesema wahitimu wao pia watachangia katika kuwezesha utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo Toleo la 2023 kuhusu mafunzo ya amali ambapo walimu mahiri wanatakiwa ili kutoa mafunzo hayo kwa ufanisi.
“Nguvu kazi yenye ujuzi
itahitajika sana katika miradi ya kimkakati kama vile uzalishaji wa nishati,
uchimbaji wa madini ya kimkakati, ujenzi wa bomba la mafuta na ujenzi wa reli
ya kisasa. Miradi yote hii itahitaji mafundi mahiri watakaozalishwa na
ninyi……,” amesema.
Dkt. Rwezimula
amewataka wahitimu hao kutambua na kutimiza vyema wajibu walionao katika
kuzalisha nguvu kazi yenye ujuzi unaohitajika katika utekelezaji wa shughuli za
kiuchumi na miradi ya kimkakati.
Kwa upande wake Mkuu
wa chuo cha MVTTC, Samweli Kaali, amebainisha kuwa miongoni mwa vipaumbele vya
chuo hicho ni kuimarisha uwezo ili kiweze kukidhi mahitaji ya walimu kufuatia
ongezeko la vyuo vya ufundi stadi nchini pamoja na mabadiliko ya Sera ya Elimu
na mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la Mwaka 2023.
Amesema chuo hicho
kimejipanga kuongeza udahili wa walimu tarajali kutoka walimu 1500 hadi kufikia
walimu 3100 ifikapo Juni 2028, sambamba na uanzishaji wa mitaala mipya 18 ya
Stashahada za Ualimu wa Ufundi na Ufundi Stadi ngazi ya 4 hadi 6 (NTA Level
4-6) katika fani sita za Kisekta ambazo ni Ujenzi, Magari, Umeme, Makenika ya
Mitambo, Sanaa Bunifu na Usindikaji Chakula.
No comments:
Post a Comment