Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), CPA Antony Kasore, amewaelekeza wasimamizi wa vyuo vipya vya VETA kuhakikisha elimu na mafunzo ya ufundi stadi yanatolewa kwa ubora.
CPA Kasore ametoa agizo hilo leo tarehe 19 Juni, 2024 alipokuwa akifunga kikao kazi kilichowakutanisha wasimamizi 30 kutoka vyuo vipya vya VETA kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa chuo cha VETA cha mkoa wa Dodoma kwa lengo la kuwajengea uwezo juu ya usimamizi na uendeshaji wa mafunzo ya Ufudi Stadi.
CPA Kasore amesema msisitizo wa VETA ni kuimarisha uendeshaji na usimamizi wa utoaji mafunzo katika ubora na viwango vinavyotakiwa ili kuzalisha wahitimu wanaokidhi mahitaji ya soko la ajira.
“tunapoendelea
kutekeleza shughuli zetu za utoaji mafunzo ni vema tukapata nafasi kama hii ya
kuweza kukumbushana misingi, sheria, kanuni na taratibu tunazopaswa kufuata na
kuziheshimu katika kuyatekeleza majukumu yetu vizuri kwa mustakabali na maslahi
mapana ya Watanzania na taifa kwa ujumla” amesema.
Akitoa shukrani kwa niaba ya wasimamizi hao, Kaimu Msajili kutoka chuo cha VETA cha Wilaya ya Ukerewe, Mhandisi Shinzeh Deudedith, amesema kikao kazi hicho kimekuwa na manufaa makubwa kwao katika kuimarisha utendaji kazi wao na kuahidi kutumia maarifa waliyoyapata ili kazi za utoaji Mafunzo ya Ufundi Stadi zifanyike kwa ufanisi na weledi zaidi.
No comments:
Post a Comment