CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Sunday, 22 January 2023

MAANDALIZI YA UJENZI WA VYUO 64 VYA UFUNDI STADI VYA WILAYA NCHINI


 Tarehe 21 Januari,2023, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa VETA,CPA Anthony Kasore amekagua kiwanja kitakachotumika kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Ufundi Stadi cha Wilaya ya Songwe ikiwa ni hatua za maandalizi ya ujenzi wa vyuo 64 vya Ufundi Stadi vya Wilaya nchini unaotarajiwa kuanza hivi karibuni!CPA Kasore aliongozana na viongozi mbalimbali wa Wilaya ya Songwe akiwemo Mbunge wa Jimbo la Songwe, Mhe. Philipo Mulugo.

Friday, 13 January 2023

VETA - Tafadhali tutumie taarifa zako ili tuweze kuhamasisha wengine kujiunga na Mafunzo ya Ufundi Stadi.


 

JE WEWE NI MHITIMU WA CHUO CHA VETA NA BAADA YA KUHITIMU VETA, UKO WAPI NA UNAFANYA NINI?


 

VETA YAJIPANGA KUFANYA MAKUBWA 2023

Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imejipanga vyema kuhakikisha watanzania wengi zaidi wananufaika na mafunzo bora ya ufundi stadi yanatolewa kupitia vyuo vyake nchini kote.

Akitoa salamu za mwaka mpya kwa Watanzania jijini Dodoma tarehe 4 Januari, 2023, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA Anthony Kasore, alisema kwa mwaka 2023 VETA imedhamiria kuongeza fursa zaidi za mafunzo ya ufundi stadi  kwa watanzania ili kuwawezesha kujipatia ujuzi utakaowawezesha kushiriki kikamilifu kwenye shughuli mbalimbali za uchumi.

CPA. Kasore ametaja baadhi ya matarajio ya Mamlaka hiyo kuwa ni kuongeza udahili wa wanafunzi kutoka 90,000 kwa mwaka 2022 hadi 118,000 kwa mwaka 2023 na kumalizia ujenzi wa vyuo 25 vya ufundi stadi vya Wilaya pamoja na kuratibu ujenzi wa vyuo vipya 64 vya Wilaya na chuo cha Mkoa wa Songwe.

“Tumejipanga vyema kuhakikisha kuwa ujenzi wa vyuo vya ufundi stadi vya Wilaya 63 nchini na ujenzi wa chuo cha ufundi stadi na huduma cha Mkoa wa Songwe unatekelezwa kwa ufanisi… Tunashukuru Serikali imeshatenga shilingi bilioni 100 katika mwaka wa fedha 2022/2023 kwa ajili ya kuanza ujenzi huo,” alisema.


Akizungumza kuhusu mafanikio yaliyopatikana mwaka 2022, CPA Kasore alitaja baadhi ya mafanikio kuwa ni pamoja na kukamilisha kwa asilimia 97 ujenzi wa vyuo 25 vya Wilaya kwa kutumia nguvu kazi ya ndani yaani “Force Account” na uratibu wa ujenzi wa vyuo vinne vya Mikoa ya Simiyu, Njombe, Geita na Rukwa. 

Katika kuhakikisha mafunzo ya ufundi stadi yanatolewa kwa ubora, CPA Kasore alisema katika mwaka 2022, jumla ya mitaala 48 ilihuishwa ili kuendana na mahitaji halisi ya soko la ajira na kuakisi mabadiliko ya sayansi na teknolojia.

Aidha, CPA Kasore alisema VETA imeendeleza ushirikiano na wadau mbalimbali ili kuwafikia watanzania wengi zaidi wenye mahitaji ya mafunzo ya ufundi stadi na kukidhi mahitaji ya makundi mbalimbali kwenye jamii.


Alitaja baadhi ya wadau hao kuwa ni Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu kupitia mradi wa Uwanagenzi ambapo jumla ya vijana 3900 walipatiwa mafunzo na Shirika la Maendeleo ya Ujerumani (GIZ) kupitia mradi wa E4D kutoa mafunzo kwa vijana 4200 nchini.Wanufaika wote hao walipatiwa mafunzo hayo bila malipo.

CPA Kasore alitoa shukrani kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa kipaumbele kikubwa kwenye elimu na mafunzo ya ufundi stadi ili kuhakikisha watanzania wanajipatia ujuzi utakaowawezesha kushiriki kwenye shughuli mbalimbali za kiuchumi na kuwezesha vijana kujiajiri.

“Mhe. Rais amekuwa na malengo makubwa sana katika kuhakikisha elimu ya ufundi stadi inaimarika na kutolewa ndani ya nchi na tumeshuhudia mengi yakifanyika kwenye eneo la kuboresha miundombinu inayotumika kutoa mafunzo ya ufundi stadi… Tunamshukuru sana,” Amesema

Kwa mujibu wa CPA Kasore, moja ya changamoto inayoikabili Mamlaka hiyo ni kushindwa kuhimili idadi kubwa ya watanzania wanaoomba nafasi za kupata mafunzo ya ufundi stadi kwenye vyuo vya VETA ambayo anaamini itatatulia kwa kiasi kikubwa na ujio wa vyuo vya Wilaya na Mikoa, huku Mamlaka hiyo ikiendelea kubuni njia mbadala za utoaji mafunzo kwa watanzania.

Usikose kufuatilia kipindi cha Ujuzi ni Maisha leo Ijumaa, tarehe 13.01.2023 saa 3:30 usiku, TBC1 tutakuwa tukionesha utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa vyuo vya ufundi stadi vya wilaya za Kilindi,Pangani, Lushoto na Mkinga, Mkoani Tanga.


 

Tuesday, 10 January 2023

MISINGI YA MAADILI YA UTENDAJI KAZI VETA


 

Bodi ya VETA yapongezwa uboreshaji na upanuzi wa utoaji mafunzo ya ufundi stadi nchini


Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Francis Michael, ameipongeza Bodi ya Nane ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi kwa usimamizi thabiti wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi nchini.

Akizungumza wakati wa hafla ya kuiaga Bodi hiyo jijini Dodoma tarehe 9 Januari, 2023, Dkt. Michael amesema miongoni mwa mambo yaliyosimamiwa vyema na Bodi hiyo ni ujenzi wa vyuo vya ufundi stadi vya wilaya ambao umetekelezwa na VETA kwa kutumia nguvukazi ya ndani, pamoja na ubunifu wa programu za mafunzo kwa kuzingatia mahitaji ya soko la ajira na mwenendo wa nchi kiuchumi.

“Itoshe kusema kwamba usimamizi wenu ulikuwa mzuri na mmeitendea vyema mipango mbalimbali ya VETA, hasa Mpango Mkakati wa Tano (VCP V) wa mwaka 2018/2019 hadi 2022/2023 ambao ndo hasa ulikuwa katika kipindi chetu cha usimamizi wa VETA… hongereni sana. ,” amesema.

Amesema Serikali ya Awamu ya Sita imeipa kipaumbele kikubwa sana elimu na mafunzo ya ufundi stadi na kwamba uendeshaji na usimamizi wake unapaswa kuwa imara na madhubuti.

Awali, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa VETA, CPA. Anthony Kasore, amesema katika kipindi cha kuanzia mwezi Februari, 2020, VETA imepata mafanikio mbalimbali ikiwemo uandaaji wa mitaala 54 kuendana na mahitaji ya soko la ajira, uanzishwaji wa vyuo vipya 19 pamoja na utanuzi wa miundombinu 31 kwenye vyuo vya VETA nchini na kuongeza udahili wa wanafunzi kwenye vyuo vya VETA kutoka 56,000 mwaka 2020 hadi 141,854 mwaka 2023.

Mwenyekiti wa Bodi ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Ndugu Peter Maduki, ameishukuru Serikali kwa kuiamini Bodi hiyo na kuipa ushirikiano mkubwa katika kutekeleza majukumu yake na hatimaye kuiwezesha VETA kupiga hatua katika utoaji wa mafunzo ya ufundi stadi.

Bodi ya Nane ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi ilianza kutekeleza majukumu yake tarehe 27 Februari, 2020 na inatarajiwa kumaliza muda wake tarehe 26 Februari 2023.