CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Saturday 20 April 2024

BARAZA KUU LA WAFANYAKAZI WA VETA LAZINDULIWA


 

BARAZA KUU LA WAFANYAKAZI WA VETA LAZINDULIWA



Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), CPA Anthony Kasore amezindua rasmi Baraza Kuu la Wafanyakazi wa VETA, leo tarehe 20 Aprili, 2024.

Akizindua baraza na kikao chake cha kwanza katika Ukumbi wa mikutano wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma, CPA Kasore amewataka watumishi wanaounda baraza kuu la wafanyakazi wa VETA, kwenda kutekeleza jukumu kubwa la utoaji Mafunzo kwa weledi kwa ajili ya matokeo chanya yenye maslahi kwa VETA na Tanzania kwa ujumla.


Amewaomba wajumbe wa baraza kusaidia katika kuwawezesha Watanzania kunufaika na VETA, kufikia malengo pamoja na kutekeleza maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwa na Watanzania wenye ujuzi utakaowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na kijamii nchini.  

 “ Tukaoneshe matokeo ya uwekezaji mkubwa uliofanywa VETA kupitia ujenzi wa vyuo  kote nchini kwa kwenda kutekeleza wajibu wetu wa kutoa ujuzi unaokidhi viwango vinavyohitajika na wananchi ili kutimiza kiu na imani kubwa walio nayo kwetu katika kuwapitia Mafunzo” alihimiza.

Nae Mwakilishi wa Kamishna wa Kazi, Ndugu Honesta Ngolly amesema vipo vyama vya wafanyakazi kama RAAWU ambao wameaminiwa na watumishi wengine katika kuwawakilisha, hivyo uzinduzi wa baraza ukawape nafasi wawakilishi hao kukaa pamoja kujadili mustakabali wa wafanyakazi ili kuwapa moyo wa kuweza kuyatekeleza yale ambayo Tanzania inatarajia kutoka VETA. 

Akishukuru kwa kuchaguliwa kuwa mwakilishi wa wafanyakazi wenye mahitaji maalumu, Bakari Athumani, mwalimu wa fani ya Uungaji na Uundaji Vyuma kutoka VETA Kanda ya Ziwa, amewataka watumishi wanaoiwakilisha VETA kushirikiana na kuwa waadilifu katika kufanya kazi ili kuyafikia malengo ya Taasisi.


Baraza hilo litadumu katika kipindi cha miaka mitatu kulingana na mkataba wa uundaji wa mabaraza ya wafanyakazi uliosainiwa kati ya VETA na Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu, Sayansi, Teknolojia, Ufundi Stadi, Habari na Utafiti (RAAWU).

Friday 19 April 2024

CPA Kasore: Kasimamieni utoaji mafunzo ya ufundi stadi kwa ubora kulingana na mahitaji ya soko la Ajira

 

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) CPA. Anthony Kasore, amewaagiza wasimamizi wa mafunzo ya ufundi stadi kwenye vyuo vya VETA kuimarisha utoaji mafunzo ya ufundi stadi kuendana na mahitaji ya soko la ajira.

CPA. Kasore ametoa maagizo hayo wakati wa kikao kilichowakutanisha wajumbe wa Menejimenti ya VETA Makao makuu, Wakurugenzi wa Kanda na wakuu wa vyuo vya VETA kilichofanyika jijini Dodoma leo tarehe 19 Aprili, 2024.

Kasore amesema Serikali imeiamini VETA kutoa mafunzo ya ufundi stadi hapa nchini, hivyo ni wajibu wa watendaji wa VETA kutekeleza jukumu hilo kwa weledi.

 “nawahimiza kwa dhati kuwa mkatimize jukumu tulilonalo la kutoa mafunzo bora kulingana na mahitaji ya soko la ajira ili tuweze kuzalisha nguvukazi ya vijana bora katika fani,” amesema

CPA Kasore ameeleza kiu yake ya kuona watumishi wa VETA wanaimarisha ubora wa mafunzo na kasi ya utoaji mafunzo ili wananchi wote wapate mafunzo hayo kwa ubora  na hatimaye kuwa na nguvukazi mahiri kwa ajili ya kushiriki kwenye shughuli za kiuchumi.






TAARIFA KWA UMMA - MABADILIKO YA MUONEKANO WA VYETI VYA UDEREVA


 

Monday 15 April 2024

MKURUGENZI MKUU WA VETA ASISITIZA USHIRIKIANO BAINA YA WAFANYAKAZI KUIMARISHA UTOAJI MAFUNZO YA UFUNDI STADI


 

MKURUGENZI MKUU WA VETA ASISITIZA USHIRIKIANO BAINA YA WAFANYAKAZI KUIMARISHA UTOAJI MAFUNZO YA UFUNDI STADI

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), CPA Anthony Kasore, amewataka wafanyakazi wa VETA kuboresha ushirikiano katika utendaji kazi ili kuimarisha utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi nchini.

CPA. Kasore ametoa wito huo tarehe 14 Aprili, 2024 katika ofisi za VETA Makao Makuu jijini Dodoma wakati wa hafla fupi iliyoandaliwa na watumishi hao ya kumpokea na kumpongeza kwa kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Mkurugenzi Mkuu wa VETA.

Amesema ushirikiano baina ya wafanyakazi wa Mamlaka hiyo utawezesha ufanisi katika kutekeleza shughuli za utoaji mafunzo hasa kwa kutambua umuhimu na mchango wa kila mmoja katika kufikia malengo yaliyowekwa.

CPA Kasore amesisitiza dhamira yake ya kuhakikisha malengo ya Serikali ya kutoa ujuzi kwa Watanzania kupitia vyuo vya VETA nchini yanafikiwa na kuwataka watumishi wa VETA kushiriki kikamilifu katika kuweka mipango na mikakati thabiti ya kufanikisha dhamira hiyo ya Serikali.

 

“Nasisitiza wote (watumishi) kutambua jukumu kubwa tulilonalo katika kuwapatia wananchi ujuzi ambao ndiyo msingi mkuu katika kuwawezesha kushiriki katika shughuli za kiuchumi zitakazowaongezea kipato na kuongeza pato la taifa kwa ujumla …Ni wajibu wetu kufanikisha utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi kwa ubora na umahiri,”amesema

Awali, Mkurugenzi wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Abdallah Ngodu amempongeza CPA Kasore kwa kuaminiwa na kuteuliwa na Mhe. Rais na kusimamia utekelezaji wa shughuli za utoaji mafunzo ya ufundi stadi zinazofanywa na VETA.

Akizungumza kwa niaba ya watumishi wa VETA, Mtunza Kumbukumbu wa VETA Makao Makuu, Hussein Rubaka amempongeza CPA. Kasore kwa kuteuliwa kuiongoza VETA na kuahidi ushirikiano katika kutekeleza majukumu yake huku wakifanya kazi kwa kujituma na kwa ufanisi ili kufikia malengo la Taasisi.

CPA Anthony Kasore aliteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania, kuwa Mkurugenzi Mkuu wa VETA, tarehe 12 Aprili, 2024 . Kabla ya uteuzi huo, CPA Kasore alikuwa akikaimu nafasi hiyo.