Saturday 20 April 2024
BARAZA KUU LA WAFANYAKAZI WA VETA LAZINDULIWA
Mkurugenzi Mkuu wa
Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), CPA Anthony Kasore
amezindua rasmi Baraza Kuu la Wafanyakazi wa VETA, leo tarehe 20 Aprili, 2024.
Akizindua baraza na kikao chake cha kwanza katika Ukumbi wa mikutano wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma, CPA Kasore amewataka watumishi wanaounda baraza kuu la wafanyakazi wa VETA, kwenda kutekeleza jukumu kubwa la utoaji Mafunzo kwa weledi kwa ajili ya matokeo chanya yenye maslahi kwa VETA na Tanzania kwa ujumla.
Amewaomba wajumbe wa baraza kusaidia katika kuwawezesha Watanzania kunufaika na VETA, kufikia malengo pamoja na kutekeleza maono ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwa na Watanzania wenye ujuzi utakaowawezesha kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi na kijamii nchini.
“ Tukaoneshe matokeo ya uwekezaji mkubwa uliofanywa VETA kupitia ujenzi wa vyuo kote nchini kwa kwenda kutekeleza wajibu wetu wa kutoa ujuzi unaokidhi viwango vinavyohitajika na wananchi ili kutimiza kiu na imani kubwa walio nayo kwetu katika kuwapitia Mafunzo” alihimiza.
Nae Mwakilishi wa
Kamishna wa Kazi, Ndugu Honesta Ngolly amesema vipo vyama vya wafanyakazi kama
RAAWU ambao wameaminiwa na watumishi wengine katika kuwawakilisha, hivyo
uzinduzi wa baraza ukawape nafasi wawakilishi hao kukaa pamoja kujadili
mustakabali wa wafanyakazi ili kuwapa moyo wa kuweza kuyatekeleza yale ambayo
Tanzania inatarajia kutoka VETA.
Akishukuru kwa kuchaguliwa kuwa mwakilishi wa wafanyakazi wenye mahitaji maalumu, Bakari Athumani, mwalimu wa fani ya Uungaji na Uundaji Vyuma kutoka VETA Kanda ya Ziwa, amewataka watumishi wanaoiwakilisha VETA kushirikiana na kuwa waadilifu katika kufanya kazi ili kuyafikia malengo ya Taasisi.
Baraza hilo litadumu
katika kipindi cha miaka mitatu kulingana na mkataba wa uundaji wa mabaraza ya
wafanyakazi uliosainiwa kati ya VETA na Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za
Elimu ya Juu, Sayansi, Teknolojia, Ufundi Stadi, Habari na Utafiti (RAAWU).
Friday 19 April 2024
CPA Kasore: Kasimamieni utoaji mafunzo ya ufundi stadi kwa ubora kulingana na mahitaji ya soko la Ajira
Mkurugenzi Mkuu wa
Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) CPA. Anthony Kasore,
amewaagiza wasimamizi wa mafunzo ya ufundi stadi kwenye vyuo vya VETA
kuimarisha utoaji mafunzo ya ufundi stadi kuendana na mahitaji ya soko la
ajira.
CPA. Kasore ametoa maagizo hayo wakati wa kikao kilichowakutanisha wajumbe wa Menejimenti ya VETA Makao makuu, Wakurugenzi wa Kanda na wakuu wa vyuo vya VETA kilichofanyika jijini Dodoma leo tarehe 19 Aprili, 2024.
Kasore amesema
Serikali imeiamini VETA kutoa mafunzo ya ufundi stadi hapa nchini, hivyo ni
wajibu wa watendaji wa VETA kutekeleza jukumu hilo kwa weledi.
“nawahimiza kwa dhati kuwa mkatimize jukumu tulilonalo la kutoa mafunzo bora kulingana na mahitaji ya soko la ajira ili tuweze kuzalisha nguvukazi ya vijana bora katika fani,” amesema
CPA Kasore ameeleza
kiu yake ya kuona watumishi wa VETA wanaimarisha ubora wa mafunzo na kasi ya
utoaji mafunzo ili wananchi wote wapate mafunzo hayo kwa ubora na hatimaye kuwa na nguvukazi mahiri kwa
ajili ya kushiriki kwenye shughuli za kiuchumi.
Monday 15 April 2024
MKURUGENZI MKUU WA VETA ASISITIZA USHIRIKIANO BAINA YA WAFANYAKAZI KUIMARISHA UTOAJI MAFUNZO YA UFUNDI STADI
Mkurugenzi Mkuu wa
Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), CPA Anthony Kasore,
amewataka wafanyakazi wa VETA kuboresha ushirikiano katika utendaji kazi ili
kuimarisha utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi nchini.
CPA. Kasore ametoa wito huo tarehe 14 Aprili, 2024 katika ofisi za VETA Makao Makuu jijini Dodoma wakati wa hafla fupi iliyoandaliwa na watumishi hao ya kumpokea na kumpongeza kwa kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa Mkurugenzi Mkuu wa VETA.
Amesema ushirikiano baina ya wafanyakazi wa Mamlaka hiyo utawezesha ufanisi katika kutekeleza shughuli za utoaji mafunzo hasa kwa kutambua umuhimu na mchango wa kila mmoja katika kufikia malengo yaliyowekwa.
CPA Kasore amesisitiza dhamira yake ya kuhakikisha malengo ya Serikali ya kutoa ujuzi kwa Watanzania kupitia vyuo vya VETA nchini yanafikiwa na kuwataka watumishi wa VETA kushiriki kikamilifu katika kuweka mipango na mikakati thabiti ya kufanikisha dhamira hiyo ya Serikali.
“Nasisitiza wote (watumishi) kutambua jukumu kubwa tulilonalo katika kuwapatia wananchi ujuzi ambao ndiyo msingi mkuu katika kuwawezesha kushiriki katika shughuli za kiuchumi zitakazowaongezea kipato na kuongeza pato la taifa kwa ujumla …Ni wajibu wetu kufanikisha utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi kwa ubora na umahiri,”amesema
Awali, Mkurugenzi wa
Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Abdallah Ngodu amempongeza CPA Kasore kwa
kuaminiwa na kuteuliwa na Mhe. Rais na kusimamia utekelezaji wa shughuli za
utoaji mafunzo ya ufundi stadi zinazofanywa na VETA.
Akizungumza kwa niaba ya watumishi wa VETA, Mtunza Kumbukumbu wa VETA Makao Makuu, Hussein Rubaka amempongeza CPA. Kasore kwa kuteuliwa kuiongoza VETA na kuahidi ushirikiano katika kutekeleza majukumu yake huku wakifanya kazi kwa kujituma na kwa ufanisi ili kufikia malengo la Taasisi.
CPA Anthony Kasore
aliteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania, kuwa Mkurugenzi Mkuu wa
VETA, tarehe 12 Aprili, 2024 . Kabla ya uteuzi huo, CPA Kasore alikuwa akikaimu
nafasi hiyo.