CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Friday, 28 July 2017

VETA yazidi kupata mvuto kwa wananchi




Maonesho ya Biashara ya Kimataifa Dar es Salaam, maarufu kama Sabasaba yamemalizika jijini Dar es Salaam Julai 13, 2017 huku Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) ikizidi kupata wingi wa wahudhuriaji katika banda lake.


Wakati maonesho ya Sabasaba yakiwa na kaulimbiu isemayo, “Ukuzaji wa Biashara kwa Maendeleo ya Viwanda,” VETA ilikoleza kwa ujumbe, “Viwanda Vinahitaji Ujuzi, Ujuzi Unapatikana VETA”

Takwimu za mahudhurio ya watu katika banda la VETA zimeonesha kuwa takribani watu 59,101 wakiwemo wageni mashuhuri 19 walitembelea banda la VETA katika kipindi chote cha maonesho kuanzia tarehe 28 Juni hadi 13 Julai, 2017, idadi ambayo imeongezeka zaidi ya mara dufu ukilinganisha na mwaka jana (2016) ambapo idadi ya wahudhuriaji  ilikuwa yapata 26,000.

Wengi wa watu waliotembelea banda la VETA walionesha kuridhishwa kwa kiasi kikubwa na huduma zake, ambapo 58,788 (96%) walisema maonesho ya huduma za VETA ni mazuri sana, 2207 (3.7) mazuri na 324 (0.54%) wastani.

Licha ya kupata watu wengi wakitembelea banda lake, VETA ilifanikiwa kuibuka mshindi katika kundi la Uendelezajii Ujuzi na Mafunzo na kuwa mshindi wa pili wa jumla wa maonesho ambayo yalishirikisha taasisi, makampuni na mashirika 2520 kutoka nchi 31.

Akizungumzia maonesho hayo, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dr. Bwire Ndazi alisema kumekuwa na mwamko mkubwa wa wananchi kutembelea banda la VETA kutokana na kutambua fursa mbalimbali za ujuzi pamoja na ubunifu ambao umekuwa ukioneshwa na VETA kila mwaka.

“idadi ya watu imekuwa ikiongezeka kila mwaka kwa sababu kila mara wanaona vitu vipya, vitu vinavutia, vinahamasisha vijana na watu wengine kuhusu ujuzi na ubunifu mbalimbali,” alisema.

Aliongeza kuwa, katika maonesho hayo, VETA ililenga pia kuonesha jinsi ambavyo imejipanga kuisaidia serikali kuandaa nguvukazi yenye ujuzi kwa ajili ya maendeleo ya viwanda.

Miongoni mwa wageni mashuhuri waliotembelea banda la VETA ni pamoja na Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe. Charles John Mwijage ambaye pamoja na mambo mengine, aliipongeza VETA kwa ujumbe mzuri unaohamasisha watu kujifunza ujuzi ili washiriki kikamilifu katika uanzishaji na uendelezaji viwanda.



Naye Rais wa Awamu ya Pili ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe Ali Hassan Mwinyi alivutiwa na maendeleo ya VETA katika kusimamia na kuendeleza ufundi stadi nchini, akisema kuwa kumekuwa na ubunifu na umahiri mkubwa unaooneshwa na wanafunzi na walimu wa ufundi stadi na akaishauri VETA kuzidi kujitangaza zaidi na kutangaza ubunifu mbalimbali ili umma uzidi kutambua umuhimu wa ufundi stadi. 








No comments:

Post a Comment