CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday, 20 July 2017

Wahitimu 102 wa Ufundi Stadi Wilaya ya Temeke wapatiwa vitendea kazi



Jumla ya vijana 102 waliohitimu mafunzo ya ufundi stadi chini ya Mradi wa Uwezeshaji Vijana Kiuchumi (YEE) wilayani Temeke, jijini Dar es Salaam wamepatiwa vifaa vya kufanyia kazi ili kuwawezesha kujiajiri.

Wahitimu waliokabidhiwa vitendea kazi chini ya mradi huo wa YEE ni wale ambao wameunda vikundi vyao na kuvisajili rasmi.

Akikabidhi vifaa hivyo kwenye hafla fupi iliyofanyika katika chuo cha VETA Dar es Salaam tarehe 18 Julai, 2017 Katibu Tawala wa Wilaya ya Temeke, Hashimu Komba alipongeza hatua hiyo na kuwataka vijana kutumia vifaa hivyo walivyovipata kuboresha shughuli zao za kiufundi kulingana na fani walizosoma, hivyo kujiingizia kipato.

Aliwataka watendaji wa Wilaya na Kata kuweka utaratibu wa kufuatilia kwa karibu vikundi hivyo na kuhakikisha vifaa vilivyotolewa vinatumika kwa malengo yaliyokusudiwa na kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili na kuwatafutia suluhisho.

“Fursa hii mliyoipata leo ni ya kipekee na mna wajibu wa kutendea haki mafunzo mliyoyapata na mkakae na kupanga matumizi sahihi ya vifaa hivi,” alisema

Komba aliahidi kuwa wilaya yake itahakikisha inawaandalia vijana hao mazingira rafiki ya kuwawezesha kufanya shughuli zao kwa kuwapatia mikopo nafuu na kuwapatia zabuni mbalimbali zinazoendana na fani zao na kuzitaka ofisi za kata kufanya hivyo ili kuunga mkono jitihada za vijana hao.

Meneja Mradi wa Plan International Adolph Jeremia alisema kuwa vifaa hivyo vyenye thamani ya Shilingi 12,613,742 vimetolewa kwa vikundi vya vijana waliohitimu  fani za Umeme Majumbani, Ushonaji, Udereva, Ufundi magari,Uchomeleaji na Uungaji vyuma na mapishi na mapambo.

Alisema vijana 155 waliohitimu kati ya 257 hawajapata fursa ya kupewa vifaa kutokana na kutojiunga katika vikundi, hivyo akawashauri  pia kujiunga na kusajili vikundi vyao ili waweze kunufaika na mpango wa kupatiwa vifaa.

Mmoja wa wanufaika wa mradi huo Anna Nkembo aliyesoma fani ya ushonaji amesema mafunzo kupitia mradi huo yamebadilisha maisha yake kwani baada tu ya kuhitimu amejiajiri na anashona nyumbani kwake na kujipatia kipato cha kujikimu.

Alisema upatikanaji wa vifaa hivyo kupitia kikundi chao cha wahitimu nane utawasaidia kufanya kazi nyingi na punde wataanza kutafuta zabuni za kushona nguo nyingi zaidi hasa sare za wanafunzi. 

Mradi wa YEE unatekelezwa kwa ushirkiano kati ya VETA, Plan International, VSO, CORDET, UHIKI na CCBRT katika mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro, Pwani, Lindi na Mtwara .













No comments:

Post a Comment