CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Tuesday 15 December 2020

Miradi ya ujenzi wa vyuo vya VETA kuongeza fursa za mafunzo kwa wananchi mkoani Arusha

Fursa zaidi za mafunzo ya ufundi stadi kwa wananchi mkoani Arusha zinatarajia kuongezeka baada ya kukamilika kwa miradi ya upanuzi wa vyuo viwili vya VETA mkoani hapo na ujenzi wa Chuo kipya cha VETA cha Wilaya ya Longido.

Akikagua maendeleo ya ujenzi wa majengo mapya katika chuo cha VETA cha Hoteli na Utalii (VETA Njiro) na Chuo cha VETA Arusha, tarehe 5 Desemba, 2020, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Dkt. Pancras Bujulu, amesema miradi ya upanuzi wa vyuo hivyo umelenga kuongeza udahili wa wanafunzi na kuboresha mazingira ya utoaji mafunzo.

Katika Chuo cha VETA Njiro, Dkt. Bujulu amesema kazi ya ujenzi wa ukumbi wa mihadhara (lecture theatre), madarasa mawili, maliwato pamoja na ukarabati wa majengo ya hoteli na utawala inaendelea ambapo kiasi cha shilingi 647, 677,362 kimetengwa kwa kazi hiyo.

Dkt. Bujulu ameainisha majengo yanayojengwa katika chuo cha VETA Arusha kuwa ni Maabara ya Kompyuta na Uhazili, karakana za Ufundi Magari na Uungaji Vyuma pamoja na bweni la wasichana lenye uwezo wa kulaza wanafunzi wa kike 80 ambapo kiasi cha shilingi milioni 604,533,040 kimetengwa kwa ajili ya kazi hiyo.

Msimamizi wa miradi hiyo, Mhandisi Method Mlay, amesema miradi hiyo ya ujenzi inatarajiwa kukamilika mwezi Machi, 2021 na kwamba ujenzi huo umefikia asilimia 60.

Katika hatua nyingine, mradi wa ujenzi wa chuo cha VETA cha Wilaya ya Longido unaotekelezwa na Chuo cha VETA Arusha kwa utaratibu wa kutumia rasilimali za ndani (Force Account) unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Januari, 2021 na kuongeza fursa zaidi za mafunzo ya ufundi stadi kwa wananchi wilayani hapo.

Dkt. Bujulu aliwasisitiza viongozi wa chuo hicho kuhakikisha ujenzi unaenda kwa kasi ili wananchi wa Wilaya hiyo waanze kunufaika na mafunzo na hatimaye kuendesha kwa tija shughuli zao za kiuchumi.

Mkuu wa Chuo cha VETA Arusha, Ndugu Bangantabona Mrefu, amesema chuo chake kitaendelea kuzidisha jitihada ili kuhakikisha ujenzi huo unakamilika kwa wakati na kwa ubora uliokusudiwa.

Chuo cha VETA cha Wilaya ya Longido ni miongoni mwa vyuo 26 vya VETA vya Wilaya vinavyojengwa nchini ikiwa ni mkakati wa Serikali kuhakikisha kila Wilaya nchini inakuwa na chuo cha VETA. Chuo cha VETA Longido kinajengwa kwa gharama ya shilingi bilioni 1.7.



No comments:

Post a Comment