CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Monday 20 November 2023

KOICA YAFANYA ZIARA VYUO VYA VETA ARUSHA NA MOSHI

Wajumbe nane kutoka Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Korea (KOICA) wametembelea vyuo vya VETA Moshi na Arusha tarehe 17 Novemba, 2023 ikiwa ni sehemu ya ziara yao katika vyuo vya VETA, yenye lengo la kujifunza na kujionea jinsi Mafunzo ya Ufundi Stadi yanavyotolewa nchini.

Ziara hiyo ya siku mbili, imefanywa na wajumbe hao katika Karakana zaidi ya 10 za vyuo hivyo, zikiwemo karakana ya Uundaji na Uchongaji Vipuri; karakana ya Ufundi wa Zana za Kilimo; Karakana ya Uungaji na Uchomeleaji vyuma; Ufundi Bomba; Ufundi Magari; Ushonaji, Ubunifu wa Mavazi na Teknolojia ya Nguo; Umeme wa Magari; Ukerezaji Vyuma; Umeme wa Majumbani na karakana ya Elektroniki.

Akizungumza kwa niaba ya wajumbe hao, Kaimu Mkurugenzi Mkazi wa KOICA nchini, Bi.Jieun Seory amesema, huo ni mwendelezo wa ziara yao ya kukusanya taarifa zitakazowasaidia katika wa Ujenzi wa chuo cha ufundi hapa nchini.

"Pamoja na kupata taarifa mbalimbali za mafunzo na kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya nchi zetu, ziara hii imekuwa sehemu ya kuendelea kujifunza zaidi mbinu zinazotumika kutoa mafunzo pamoja na kufahamu uhusiano uliopo kati ya sekta ya utoaji Elimu na Mafunzo na Sekta ya viwanda, ambapo utatupa mwongozo katika uanzishwaji wa chuo  kitakachotoa mafunzo ya Ufundi kuanzia ngazi za Shahada," amefafanua.

Akiwashukuru kwa ujio wao katika vyuo vya VETA Moshi na Arusha, Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Kaskazini, Bi.Monica Mbelle, amewataka wajumbe hao kuendelea kutembelea vyuo vya VETA ili kufahamu zaidi kuhusu mafunzo yatolewayo na vyuo hivyo nchini na kubaini maeneo ya ushirikiano.

"Tuna Kanda tisa zenye vyuo vinavyotoa mafunzo tofauti tofauti nchi mzima, na kwa kuwa ziara hii imewafanya kuwa sehemu ya familia ya VETA ni vyema sasa mkapanga kutembelea vituo vingine kupata uelewa wa kina kuhusu Mafunzo yatolewayo na vyuo hivyo," ameongeza.

Naye Mkurugenzi Msaidizi wa Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Erick Mgaya, amesema, Wizara iko tayari kushirikiana na KOICA ili kuhakikisha wanafikia lengo la Utoaji mafunzo ya Ufundi Stadi nchini, hasa ikizingatiwa kwamba sasa ndio msisitizo wa Serikali ya Awamu ya Sita.

Ziara ya wajumbe hao ilitembelea pia kiwanda cha kuzalisha na kusambaza genereta za Umeme, TANELEC kilichopo eneo la Themi, jijini Arusha ambacho kwa mujibu wa ripoti ya Meneja Uendeshaji wa kiwanda hicho, Ndg. Edrick Mwenda zaidi ya asilimia 60 ya wafanyakazi wa kiwanda hicho ni wahitimu wa vyuo vya VETA nchini katika fani za Ukerezaji vyuma, Uundaji na Uungaji vyuma na Umeme wa majumbani na viwandani.

No comments:

Post a Comment