CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday 23 May 2024

WADAU SEKTA YA MADINI WAOMBWA KUFADHILI MAFUNZO YA UFUNDI STADI

 

Wito umetolewa kwa makampuni na wadau wa sekta ya madini kujitokeza kufadhili mafunzo ya ufundi stadi yanayotolewa na VETA chini ya programu maalum ya Mafunzo Jumuishi kwa ajili ya Sekta ya Madini (IMTT).

Wito huo umetolewa na Rais wa Chemba ya Biashara, Viwanda na Kiliomo Tanzania (TCCIA), Vicent Bruno Minja, wakati wa mdahalo wa siku ya kwanza ya Jukwaa la Tatu la Ushirikishwaji wa Tanzania katika Sekta ya Madini, linalofanyika ukumbi wa AICC, Jijini Arusha, tarehe 22 hadi 24 Mei, 2024.

Kwa kutambua umuhimu wa mafunzo hayo, Minja ameishauri Serikali na wadau wa madini kuona ni namna gani mafunzo hayo yanaweza kuendelezwa na kuenezwa katika vyuo vingine badala ya kuishia kwenye chuo cha VETA Moshi pekee, ambacho sasa kinatekeleza mpango huo wa mafunzo.

“Nashauri Mwanza na Mbeya na wao wawezeshwe kutoa kozi zinazohusiana na masuala ya madini kuliko kuiachia Moshi peke yake,” amesema.

Akifungua Kongamano hilo, Waziri wa Madini, Anthony Mavunde ametoa rai kwa Watanzania kuchangamkia fursa mbalimbali zilizopo katika sekta ya madini.

Maonesho hayo yanakwenda sambamba na maonesho ya shughuli na huduma mbalimbali zinazohusiana na sekta ya madini ambapo VETA inashiriki kwenye kongamano pamoja na maonesho.

Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Kaskazini, Monica Mbele, amemwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa VETA kwenye hafla ya ya ufunguzi.

VETA inatumia maonesho hayo kutoa taarifa mbalimbali za mafunzo ya Ufundi Stadi, hususani yale yanayolenga kuandaa nguvukazi yenye ujuzi kwa ajili ya Sekta ya madini kama yanavyotolewa katika vyuo vyake vya Moshi na Shinyanga.



No comments:

Post a Comment