CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Friday, 7 August 2026

PROF. MCHOME AHIMIZA USHIRIKIANO WA TAASISI KUENDELEZA UBUNIFU


Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), Profesa Sifuni Mchome, amezitaka taasisi za Serikali kuimarisha ushirikiano katika kuendeleza bunifu zinazozalishwa nchini ili zifikie hatua ya kuzalishwa kibiashara, kuongeza ajira na kuchochea ukuaji wa uchumi kuelekea utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Profesa Mchome ametoa wito huo, tarehe 5 Agosti 2026, alipotembelea banda la VETA katika Maonesho ya Kitaifa ya Kilimo (Nanenane) yanayoendelea katika Viwanja vya Nzuguni, jijini Dodoma.

Baada ya kutembelea mabanda mbalimbali ya taasisi za Serikali, amesema ameridhishwa na kiwango cha ubunifu kinachoendelea kufanywa nchini na kusisitiza kuwa ushirikiano wa taasisi hizo ni nguzo muhimu ya kuhakikisha bunifu hizo zinakuzwa na kuwanufaisha wananchi pamoja na uchumi wa taifa.

"Nimefurahi kupata nafasi ya kutembelea mabanda mbalimbali na kujionea bunifu zinazofanywa na taasisi za serikali. Nimeona bunifu za hali ya juu. Haya yanaonyesha kuwa Tanzania ina uwezo mkubwa wa ubunifu," amesema.

Akizungumzia kaulimbiu ya Maonesho ya Nanenane mwaka huu isemayo, "Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050," Prof. Mchome amesema inalenga kuwahamasisha wadau wa uzalishaji kutambua fursa za masoko, kuongeza thamani ya bidhaa na kuimarisha mnyororo wa thamani kupitia ushirikiano.




No comments:

Post a Comment