CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Friday 23 March 2018

Jitihada za Ufundi Stadi kuelekea uchumi wa viwanda



 Ujenzi wa vyuo na karakana za mafunzo maeneo mbalimbali nchini

Ukarabati vyuo na uboreshaji karakana za mafunzo

Ni Miaka miwili imetimia tangu serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mh. Rais Dkt John Pombe Magufuli, iingie madarakani. Msisitizo na mwelekeo wa Mh. Rais  na serikali yake, kama yalivyo malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025 na azma ya Mpango wa II wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2016/17-2020/21, ni kuifanya Tanzania kuwa nchi ya uchumi wa kati unaotegemezwa na viwanda. Miongoni mwa mikakati muhimu ni kuhakikisha kunakuwepo nguvukazi ya kutosha na yenye uwezo wa kuendesha shughuli mbalimbali za kiuchumi ili kufikia malengo hayo ya kitaifa.

Hivyo kuwa na nguvukazi yenye ujuzi ni suala muhimu mno na lisiloepukika, kwani ndilo huchangia kwa kiasi kikubwa katika kuhakikisha shughuli za uzalishaji na uendeshaji wa viwanda zinafanyika kwa ufanisi na kwa tija. Vilevile, ujuzi utawawezesha wananchi kuingia katika sekta rasmi ya kiuchumi ikiwa ni pamoja na kujiajiri kwa kuanzisha viwanda vidogovidogo katika vikundi au wakiwa mmoja mmoja. Umuhimu zaidi na wa kipekee ni kwa kundi lenye ujuzi wa ufundi stadi, kwani hili ndo kundi kubwa linalohitajika katika kuendesha shughuli viwandani. Hapa ndipo jukumu la Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) linapojidhihirisha.

VETA ikiwa ndio yenye dhamana ya kuandaa mafundi stadi, inatambua  kuwa katika kipindi hiki kunahitajika mikakati thabiti ya kupanua wigo na kuimarisha ubora wa mafunzo ili kwenda sambamba na mahitaji ya kuanzisha na kuendeleza viwanda.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Bwire Ndazi anabainisha mikakati mbalimbali ambayo VETA inaendelea kuipanga na kuitekeleza ili kuendelea kuongeza uzalishaji wa nguvukazi yenye ujuzi katika ufundi stadi.

“Matamanio yetu ni kuhakikisha kuwa kila Mtanzania mwenye fursa kuhitaji fursa ya elimu na mafunzo ya ufundi stadi nchini anaipata katika ubora unaohitajika ili kujenga nguvukazi yenye ujuzi na umahiri itakayoiwezesha nchi kufikia azma ya Mpango wa II wa Taifa wa Miaka Mitano (FYDP II) kujenga chumi wa viwanda,” Dkt. Ndazi anafafanua.

Anaeleza kuwa, moja ya maeneo muhimu yanayotiliwa mkazo na VETA ni kuendelea kujenga, kukarabati na kuimarisha vyuo na karakana za mafunzo katika maeneo mbalimbali ili vijana na wananchi wengi kwa ujumla waweze kupata fursa za mafunzo kwa urahisi. Mataraji ni kuongeza vyuo vinavyomilikiwa na VETA kutoka 28 mwaka 2015 hadi41 kufikia mwaka 2019. Vilevile, kujenga karakana na kuboresha zilizopo, pamoja na kukarabati vyuo vilivyopo.
“Hadi sasa, kuna mipango ya miradi zaidi ya ishirini inayohusisha ujenzi, ukarabati na uboreshaji na uimarishaji wa karakana za mafunzo,” anasema Dkt. Ndazi.

Anaitaja baadhi ya miradi hiyo kuwa ni pamoja na ujenzi wa vyuo vya mikoa vinne (4), katika mikoa ya Rukwa, Geita, Simiyu na Njombe, miradi ambayo iko katika hatua mbalimbali. Vilevile ujenzi wa vyuo vipya sita (6) katika wilaya za Ukerewe, Nyasa, Namtumbo, Kilindi, Chunya, na Chato na ukarabati vyuo viwili (2) vya wilaya za Karagwe na Korogwe pia uko katika hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na ujezi wa misingi, kuta, uezekaji, utoaji zabuni na uingiaji mikataba.  

Dkt. Ndazi anataja baadhi ya mafanikio ya hivi karibuni katika juhudi za ujenzi na ukarabati wa vyuo kuwa ni pamoja na kukamilisha  ukarabati wa chuo cha Ufundi Stadi Busokelo, Mkoani Mbeya kilichhoanza kutoa mafunzo Machi, 2017 katika fani za umeme, useramala na ushonaji. Vilevile, VETA ilikarabati Chuo cha Ufundi stadi Nkowe, wilaya ya Ruangwa, mkoani Lindi na kukiwezesha chuo kuendeleza mafunzo katika mazingira bora zaidi.
“Katika kuzidi kuimarisha na kuboresha mafunzo ya vitendo, ambayo ndiyo nguzo kuu ya ufundi stadi, suala la uboreshaji wa karakana nalo tunalipa kipaumbele kikubwa,” anaeleza Dkt. Ndazi na kuongeza, “tunajenga karakana na kununua vifaa mbalimbali vya mafunzo ili viweze kutumiwa na walimu na wanafunzi katika masomo ya vitendo.”

Anazitaja juhudi za uboreshaji na uimarishaji wa karakana kuwa ni pamoja na ujenzi wa Karakana ya kisasa ya Useremala katika Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi Dodoma (VETA Dodoma)  ambayo imekamilika kwa zaidi ya asilimia 90; Ujenzi wa karakana za Useremala na umeme wa Magari Chuo cha Mkoa Morogoro-Kihonda ambao uko katika hatua ya ukamilishaji; na ujenzi wa Karakana ya Umeme wa Viwandani katika Chuo cha Ufundi Stadi cha Mkoa-VETA Mwanza ambao uko katika hatua ya kuezeka.

Anaongeza kuwa, Mamlaka inasambaza  vifaa vya kufundishia na kujifunzia katika Vyuo vya Ufundi Stadi vya Kihonda-Morogoro, Oljoro-Arusha, Kasulu-Kigoma, Mbeya na Chuo cha Walimu wa Ufundi Stadi Morogoro (MVTTC) na inatarajia kufanya hivyo pia katika vyuo vya Singida na Iringa na kwenye karakana ya Useremala ya Chuo cha VETA Dodoma.

Dkt. Ndazi anaeleza kuwa VETA inatambua kuwa ujenzi wa vyuo, karakana na uwekaji wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia ni wa gharama kubwa na hivyo ni vigumu kumudu kujenga vyuo vingi katika maeneo mbalimbali kwa muda mfupi. Kwa hiyo, ili kukabiliana na mahitaji makubwa ya mafunzo, Mamlaka inabuni mbinu na mifumo mingine za kupanua fursa za mafunzo ya ufundi stadi sambamba na ujenzi wa vyuo.

Miongoni mwa mbinu hizo ni pamoja na kuimarisha mfumo wa mafunzo ya nje ya chuo kwa Chuo cha Walimu wa Ufundi Stadi Morogoro (MVTTC); utoaji wa kozi fupifupi za ufundi stadi; kuhamasisha na kuimarisha ushiriki wa sekta binafsi katika kuwekeza katika utoaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi kwa kukaribisha ushirikiano  pamoja na kutumia teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) kama vile mitandao ya simu kutoa mafunzo. Pia kutekeleza mwongozo wa Kitaifa wa Uwanagenzi (Apprenticeship) kwa kupanua utoaji wa mafunzo yanayohusisha chuo na mahala pa kazi kutoka katika chuo cha Moshi, Dar es Salaam na Mwanza hadi nchi nzima.

Dkt. Ndazi anaeleza baadhi ya matarajio ya kupanua wigo wa fursa za mafunzo kwa kutumia mifumo mbalimbali ya mafunzo kuwa ni pamoja na kupanua Mpango wa Kutambua na Kurasimisha Ujuzi Uliopatikana Nje ya Mfumo Rasmi  kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Bunge, Sera, Kazi, Vijana na Wenye Ulemavu kwa kufikia mafundi 4,000 ifikapo mwaka 2019;  Kuendelea kutekeleza Mpango wa Kukuza Ujuzi kwa wafanyakazi walio katika ajira rasmi viwandani kupitia mpango wa Skills Enhancement Programme (SEP) katika makampuni 50 ifikapo, 2019; na Kutoa mafunzo kwa wajasiriamali 3,000 kwa lengo la kuboresha stadi za kazi katika sekta isiyo rasmi kupitia mpango wa Integrated Training for Entrepreneurship Promotion (INTEP ifikapo mwaka 2019.

No comments:

Post a Comment