CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Thursday 20 December 2018

VETA yaanzisha ushirikiano na Chuo cha Henan-China


Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imesaini makubaliano ya kuanzisha ushirikiano kati yake na Chuo cha Henan cha Ufundi Stadi wa Kilimo lengo la kuboresha utoaji wa mafunzo kwa njia ya kutembeleana na kubadilishana ujuzi na maarifa kwa walimu na wanafunzi na shughuli zingine za kitaaluma.

Makubaliano hayo ya awali yaliafikiwa na kusainiwa (tarehe 20 Desemba 2018) kati ya Makamu wa Rais wa Chuo cha Henan cha Ufundi Stadi wa Kilimo, Profesa Dou Ruimu kwa upande mmoja na Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dr. Pancras Bujulu kwa upande mwingine na kwamba yatafuatiwa na utiaji saini wa Waraka wa Makubaliano (MoU) siku za mbeleni.

Utiaji saini wa makubaliano ya awali uishuhudiwa na Mkurugenzi wa Mafunzo na Ufundi Stadi (TVET), Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Noel Mbonde na Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VET Board), Peter Maduki, wawakilishi wa Chuo cha Henan na Wajumbe wa Menejimenti ya VETA.

VETA ina nia ya kuimarisha mafunzo katika sekta ya kilimo na miongoni mwa malengo yake ni kukiimarisha na kukiboresha chuo cha VETA Kihonda ili kiweze kubobea na kuwa kituo bora cha mfano katika mafunzo ya ufundi stadi kwenye sekta ya kilimo.

Kabla ya kusaini makubaliano, ujumbe wa watu sita kutoka Chuo cha Henan cha Ufundi Stadi wa Kilimo ukiwahusisha watendaji wakuu na wataalam mbalimbali umekuwepo nchini tangu Jumanne tarehe 18 Desemba 2018 ambapo ulifanya majadiliano na Menejimenti ya VETA Makao Makuu, ikiongozwa na Mkurugenzi Mkuu Dkt Pancras Bujulu na Jumatano, tarehe 19 Desemba 2018 ulitembelea ofisi ya VETA Kanda ya Mashariki, kisha chuo cha VETA Kihonda na kujionea karakana, mashine na vifaa mbalimbali vinavyotumika kufundishia fani ya Ufundi wa Zana za Kilimo (Agro-mechanics), mafunzo ambayo yanagusa sekta ya kilimo ambayo ndio mkondo wa chuo cha Henan.

Akizungumza kabla ya kutiwa saini makubaliano hayo ya awali, Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VET Board), Peter Maduki alisema Bodi yake inaunga mkono ushirikiano huo kutokana na kutambua umuhimu wake wa uwezekano wa kuchangia kuboresha mafunzo kwenye sekta ya kilimo ambayo ni ya msingi katika uchumi wa nchi. 

“Zaidi ya asilimia 70 ya wa Watanzania wanategemea kilimo, kwa hivyo kuboresha mafunzo kwenye kilimo maana yake ni kuboresha maisha ya Watanzania,” alisema.

Aliongeza kuwa hata katika mkakati wa sasa wa nchi kuelekea kwenye uchumi wa viwanda, kuboreshsa ujuzi katika kilimo ni sawa na kuhakikisha upatikanaji wa malighafi kwa ajili ya viwanda kwa kuwa viwanda vingi vya nchi zinazoendelea kama Tanzania hutegemea zaidi malighafi kutokana na mazao ya kilimo. 

Vilevile, Mkurugenzi wa Mafunzo na Ufundi Stadi (TVET), Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Noel Mbonde aliahidi kusaidia uharakishwaji wa ushirikiano huo kwa kuwa una fursa kubwa ya kuboresha utoaji wa mafunzo ambao ndio eneo analosimamia.

Kwa sasa mafunzo ya ufundi stadi katika vyuo vinavyomilikiwa na visivyomilikiwa na VETA hutolewa katika kozi za Ufundi wa Zana za Kilimo, Teknolojia ya Usindikaji wa Nyama, Usindikaji wa Mbegu za Mafuta, Kilimo cha Bustani na Mazao ya Nafaka, Uhudumu wa Misitu, Uokaji, Kilimo cha Uyoga, Utengenezaji wa Mvinyo, Usindikaji wa Mboga na Matunda, Usindikaji wa Samaki na Usindikaji wa Asali.

Kwa upande mahsusi wa vyuo vinavyomilikiwa na VETA, mafunzo ya muda mrefu ambayo ni ya kipindi cha miaka miwili hadi mitatu hutolewa katika fani za Ufundi wa Zana za Kilimo (VETA Kihonda, VETA Manyara, VETA Arusha-Oljoro, VETA Mpanda na VETA Dakawa); Ufugaji (VETA Singida); Teknolojia ya Usindikaji wa Nyama (VETA Dodoma). Vilevile VETA huendesha kozi za muda mfupi ambazo ni za kati ya miezi miwili hadi sita kupitia programu yake ya Uboreshaji Ujuzi kwa Wajasiriamali kwenye Sekta Isiyo Rasmi (INTEP) ukihusisha mafunzo mbaimbali kama Kilimo cha Uyoga, Ufugaji wa Samaki, Utengenezaji Mvinyo, Usindikaji wa Mboga na Matunda, Usindikaji wa Samaki na Usindikaji wa Asali.

Chuo cha Henan cha Ufundi Stadi wa Kilimo (Henan Vocational College of Agriculture) kilianzishwa mwaka 1952. Chuo hicho kilichopo katika jimbo la Henan kinachomilikiwa na serikali ya China ni chuo cha mfano katika utoaji wa elimu ya ufundi stadi katika fani ya kilimo ikiwa ni pamoja na kilimo cha bustani na mbogamboga, ufugaji na usindikaji wa chakula.

No comments:

Post a Comment