CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Wednesday 19 December 2018

VETA YAJADILIANA NA CHUO CHA HENAN-CHINA KUSHIRIKIANA KUTOA MAFUNZO SEKTA YA KILIMO


Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) iko katika majadiliano na Chuo cha Henan cha Ufundi Stadi wa Kilimo cha nchini China (Henan Vocational College of Agriculture) kuona uwezekano wa kushirikiana katika utoaji mafunzo ya ufundi stadi katika sekta ya kilimo nchini.

Ujumbe wa watu sita kutoka Chuo cha Henan cha Ufundi Stadi wa Kilimo ukiwahusisha watendaji wakuu na wataalam mbalimbali umekuwepo nchini tangu jana, Jumanne tarehe 18 Desemba 2018 ambapo ulifanya majadiliano na Menejimenti ya VETA Makao Makuu, ikiongozwa na Mkurugenzi Mkuu Dkt Pancras Bujulu. 

 Leo Jumatano, tarehe 19 Desemba 2018 ujumbe huo ulitembelea ofisi ya VETA Kanda ya Mashariki, kisha chuo cha VETA Kihonda na kujionea karakana, mashine na vifaa mbalimbali vinavyotumika kufundishia fani ya Ufundi wa Zana za Kilimo (Agro-mechanics), mafunzo ambayo yanagusa sekta ya kilimo ambayo ndio mkondo wa chuo cha Henan. 


Miongoni mwa maeneo muhimu ya ushirikiano ambayo VETA inayapendekeza ni kuimarisha chuo cha VETA Kihonda ili kiweze kubobea na kuwa kituo bora cha mfano katika mafunzo ya ufundi stadi kwenye sekta ya kilimo.
Mambo mengine ni kubadilishana teknolojia, mafunzo kwa walimu, na kutembeleana kwa walimu na wanafunzi kwa ajili ya kubadilishana ujuzi na maarifa (exchange visits). 

Kesho, Alhamisi ujumbe huo unatarajiwa kukutana na kufanya majadiliano na viongozi waandamizi wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia  pamoja na Mwenyekiti wa Bodi ya Taifa ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Peter Maduki. 

Chuo cha Henan cha Ufundi Stadi wa Kilimo (Henan Vocational College of Agriculture) kilianzishwa mwaka 1952. Chuo hicho kilichopo katika jimbo la Henan kinachomilikiwa na serikali ya China ni chuo cha mfano katika utoaji wa elimu ya ufundi stadi katika fani ya kilimo ikiwa ni pamoja na kilimo cha bustani na mbogamboga, ufugaji na usindikaji wa chakula.

No comments:

Post a Comment