CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Friday 24 May 2019

Waajiri sekta ya umma wakumbushwa kushirikisha wafanyakazi


Waajiri wa sekta ya umma nchini wamekumbushwa umuhimu wa kushirikisha wafanyakazi katika kujadili, kupanga na kufanya maamuzi ya mambo mbalimbali katika taasisi zao.

Wito huo umetolewa na Naibu Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Dkt. Michael Francis wakati akifungua Baraza Kuu la Wafanyakazi wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA), tarehe 18 Mei 2019.

Akizungumza katika kikao hicho kilichofanyika katika Ofisi za VETA Makao Makuu jijini Dar es Salaam, Dkt. Francis alisema kuwa miongoni mwa namna za kushirikisha wafanyakazi katika mipango na maamuzi ni kupitia Mabaraza ya Wafanyakazi Sehemu za Kazi ambayo yapo kwa mujibu wa sheria na kwamba lengo kuu la kuanzishwa kwake ni dhana ileile ya ushirikishwaji wa wafanyakazi.

Alisema, Mabaraza ya Wafanyakazi Sehemu za Kazi yanatoa fursa bora ya majadiliano, ushirikiano na ushirikishwaji katika maamuzi kwa kuwa yanaundwa na utatu unaohusisha Menejimenti za Taasisi; Serikali, (hususani kupitia Wizara yenye dhamana ya Kazi na Ajira); na Wafanyakazi kupitia uwakilishi wa maeneo mbalimbai ya sehemu za kazi na vyama vyao vya wafanyakazi.

Aliongeza kuwa waajiri pia wanatakiwa kuwa walinzi na kimbilio la wafanyakazi pamoja na kuwapa motisha ili kuwasaidia kuongeza ufanisi katika kazi zao.

“Menejimenti wapeni fursa wafanyakazi, muwasikilize, fungueni milango kwa wafanyakazi na wapeni motisha. Hiyo husaidia kuwafanya wafanyakazi wapende kazi na kuongeza bidii ambayo inaleta tija kazini,” Alisema.

Kwa upande mwingine, Dkt. Francis aliwakumbusha wafanyakazi kutii mamlaka na kutimiza wajibu wao kazini, kwani mishahara wanayolipwa ni kwa ajili ya kufanya kazi na si vinginevyo.

Akitoa shukrani kwa Mgeni Rasmi, Mkurugenzi Mkuu wa VETA Dkt. Pancras Bujulu aliiomba Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma kuikumbuka VETA na kuipa kipaumbele inapoomba nafasi za kuajiri, kwani taasisi ni kubwa na inazidi kupanuka, hivyo mahitaji ya wafanyakazi sasa ni makubwa.

Aliongeza kuwa VETA inachukua muda mrefu kuandaa walimu wa kufundisha ufundi stadi na wanapostaafu huacha pengo kubwa, kwani watu wenye ujuzi wa kufundisha ufundi stadi kujaza nafasi zilizoachwa wazi huwa ni shida kuwapata, hivyo kuiomba serikali kufikiria namna ya kusaidia kukabiliana na changamoto hiyo.  


No comments:

Post a Comment