CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Monday 20 May 2019

VETA Kihonda yatoa mafunzo kwa madereva wa magari makubwa zaidi ya 1500


Chuo cha VETA Kihonda kimetoa mafunzo kwa madereva wa magari makubwa zaidi ya 1500 kwa kipindi cha kuanzia mwezi Januari mwaka huu lengo likiwa ni kupunguza ajali ambazo zinatokana na makosa ya kibinadamu.

Chuo cha VETA Kihonda ni Chuo ambacho kimebobea katika utoaji wa mafunzo ya udereva magari makubwa ambapo madereva wa magari makubwa wanatakiwa kupata mafunzo hayo hapo au vyuo vingine vilivyosajiliwa vikiwa na mafunzo hayo.

Mwalimu wa Udereva wa Magari Makubwa na Mabasi wa chuo cha VETA Kihonda William Munuo amesema kuwa madereva wengi wanajua kuendesha kwa kunyoosha katika barabara lakini kurudi nyuma ni tatizo ambapo wengi ndio wanasababisha ajali au kuangusha magari hayo na kuleta hasara kwa makampuni.

Munuo amesema mafunzo waliyoyaanza ni endelevu na kutaka madereva kuzingatia mafunzo hayo na kuyaishi katika kuendesha na hatimaye watakuwa madereva bora.

Munuo amesema mafunzo hayo yanafanya magari makubwa kuishi muda mrefu kutokana na wakati mwingine yanapata ubovu kwa uendeshaji usiofuata utaratibu wa uendeshaji wa magari hayo.

Amesema kuwa licha ya kuwa na leseni madereva wa magari makubwa wanahitaji mafunzo ya mara kwa mara kutokana na teknolojia za magari kubadilika kila mara.

Aidha amesema katika mafunzo ya vitendo baadhi wanajua kuendesha magari makubwa ya tela moja wengine ni wale wa tela mbili ambapo wanaweza wote kuendesha lakini wakiwekwa katika urudishaji gari hizo nyuma kuna changamoto hivyo changamoto hizo zinatatuliwa kwa kuwapa mafunzo.

"Hatuwezi kuwaacha watu waendelee kuendesha magari makubwa katika ujuzi wa mazoea lazima wapate mafunzo bora ya kuweza kuwa madereva bora na sio bora madereva"amesema Munuo.

Munuo ameyataka makampuni kuhakikisha madereva wao wanapata mafunzo kila mara kwa faida ya kampuni hizo na kusaidia utunzaji wa magari hayo.











No comments:

Post a Comment