CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Friday 13 December 2019

Ufundi Stadi Kufundishwa kwa Lugha ya Kiswahili


Katika lengo la kuendelea kupanua wigo na fursa za upatikanaji wa elimu na mafunzo ya ufundi stadi nchini, Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imetafsiri Mitaala ya fani 24 na Mihtasari 16 katika lugha ya Kiswahili.

Mitaala na Mihtasari hiyo imekabidhiwa rasmi leo, tarehe 13 Desemba, 2019 kwa Naibu Katibu Mkuu (E), Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Ave Maria Semakafu, na inatarajiwa kuanza kutumika kufundishia ufundi stadi katika Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi (FDC) nchini. 

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo kwenye ofisi za VETA Makao Makuu Jijini Dar es Salaam, Dkt. Semakafu aliipongeza VETA kwa kukamilisha kazi hiyo na kusema kuwa ufundishaji kwa Kiswahili kutawawezesha wananchi wengi, kujifunza na kuelewa vyema mafunzo hayo.

Alisema, wapo watu wengi walioamua kujifunza ufundi stadi katika mfumo usio rasmi kwa sababu ya changamoto ya lugha inayotumika kufundishia, kwani wengi wao wana ugumu kufuatilia vyema mafunzo yanayotolewa kwa lugha ya Kiingereza.  

“Tunakwenda kwenye Uchumi wa Viwanda. Inabidi tukubali kubadilika. Matumizi ya Mitaala ya Kiswahili iwe hatua ya kwanza. Kuna mengi ya kuboresha. Tufungue milango ili tupokee mawazo mapya na kuyafanyia kazi. Ufundi Stadi uwe mkombozi kwa jamii nzima ya Watanzania, hata wanaoendesha shughuli zao za kifundi mitaani,” alisema Dkt. Semakafu.

Aliishauri VETA kuchambua na kuona kama kuna haja ya kuwa na kundi la wale wanaotaka kujifunza kwa Kiingereza kwa lengo la kuendelea na masomo ya juu zaidi, lakini mafunzo ya jumla yatolewe kwa lugha ya Kiswahili. 

Akitoa taarifa kwa Naibu Katibu Mkuu, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu alisema jumla Mitaala 24 na Mihtasari 16 imetafsiriwa kwa lugha ya Kiswahili, ambapo nakala 240 zimechapishwa kwa kila kitabu, hivyo kufanya jumla ya nakala za Mitaala na Mihtasari zilizoshachapwa kuwa 9,600.




No comments:

Post a Comment