CONTACT US: VETA Head Office, P.O.Box 802 Dodoma Tanzania, Plot No. 18, Central business Park (CBP). E-mail: info@veta.go.tz / pr@veta.go.tz/ Telephone: +255 26 2963661 Mobile +255 755267489 Fax: +255 22 2863408 / Url: www.veta.go.tz

Sunday 8 March 2020

VETA yatembelea VTA Zanzibar


Tarehe 5 Machi, 2020, viongozi wa Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Satadi (VETA) walitembelea Mamlaka ya Mafunzo ya Amali (VTA) Zanzibar kujionea shughuli mbalimbali za Ufundi stadi zinazofanyika visiwani humo.

Ziara hiyo ni mwitikio wa mwaliko uliotolewa na VTA kwa VETA baada ya VTA kutembelea VETA mnamo tarehe 13 Februari, 2020 kwa lengo la kuongeza uelewa juu ya taratibu za usajili, utoaji ithibati na uendeshaji wa vyuo vya amali (ufundi stadi).

Mkurugenzi Mkuu wa VETA Dkt. Pancras Bujulu aliongozana na Kaimu Mkurugenzi wa Mafunzo, Bi. Stella Ndimubenya, na Kaimu Mkurugenzi wa VETA Kanda ya Dar es Salaam, Bi. Florence Kapinga, ambao walitembelea ofisi za VTA na kukutana na Mkurugenzi Mkuu wa VTA, Dkt. Bakari Ali Silima.

Katika mazungumzo yao, Mkurugenzi Mkuu wa VETA, Dkt. Pancras Bujulu, alisema kuwa VETA itaendelea kuimarisha ushirikiano na VTA kwa kuwa Taasisi hizo zina jukumu linalofanana la kuandaa nguvukazi inayotakiwa kujenga Taifa kuelekea  uchumi wa kati kupitia maendeleo ya viwanda.


“Naamini tutashauriana na kusaidiana masuala tofauti tofauti yanayohusu utoaji wa mafunzo ya ufundi stadi kwa vijana, hasa kuhakikisha kuwa tunatoa mafunzo yenye ubora unaolingana”, alisema.



Kupitia ziara hiyo viongozi wa VETA walipata fursa ya kutembelea vyuo vinavyotoa mafunzo ya amali vya Taasisi ya Sayansi na Teknolojia Karume na Chuo cha Mafunzo ya Amali Machui kinachomilikiwa na kanisa Katoliki. Viongozi hao wa VETA walipata fursa ya kutembelea maonesho na kuhudhuria hafla ya ufunguzi wa Juma la Mamlaka ya Mafunzo ya Amali ambapo Mgeni Rasmi alikuwa ni Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali wa Zanzibar Mhe. Riziki Pembe Juma.

Mkurugenzi Mkuu wa VTA Dkt. Bakari Silima aliwashukuru viongozi hao wa VETA kwa kufika Zanzibar na kushiriki uzinduzi huo na kusisitiza umuhimu wa kudumisha mshikamano uliopo baina ya Taasisi hizo mbili ili kuhakikisha vijana mahiri wenye ujuzi wanazalishwa kwa wingi na kuchangia katika maendeleo ya nchi.


Baada ya uzinduzi, viongozi hao wa VTA na VETA walipata fursa ya kuchambua rasimu ya Randama ya Makubaliano kwa ajili ya ushirikiano baina ya Taasisi hizo mbili ambayo inatarajiwa kusainiwa siku za karibuni. 



No comments:

Post a Comment